1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

"Je, hilo ndilo suluhisho?"

29 Machi 2007

Mzozo kati ya Uingereza na Iran juu ya wanamaji 15 walishikwa na Iran unazidi kuwa mkali. Katika uchambuzi wake juu ya mzozo huu, mwandishi wetu anasema diplomasia kimya kingesaidia zaidi.

https://p.dw.com/p/CHHA

Mzozo uliozuka kati ya Uingereza na Iran unaonyesha jinsi serikali ya Uingereza vile vile nchi zote za Magharibi zilivyoshikwa katika hali ya mtanziko. Kwa upande mmoja zinatumia maneno makali katika mzozo juu ya mpango wa kinyuklia wa Iran na kuonya kuiwekea vikwazo Iran ambavyo lakini havina uzito. Na pia katika hoja hii ya wanamaji 15 waliokamatwa au kutekwa nyara nchini Iran. Kwanza waziri mkuu wa Uingereza, Tony Blair, alitisha kuchukua hatua kali, lakini kilichofanyika ni kusitisha tu mahusiano na Iran, maana yake hakuna ziara rasmi nchini Iran wala biashara kati ya Iran na Uingereza. Je, hilo ndilo suluhisho?

Bila shaka, ni jambo zuri kwamba diplomasia ya kutumia meli za vita haitumiki tena. Ni maneno tu ya wanasiasa ambayo ni makali, lakini hatua yao sio kali tena. Zamani huenda tukio hili la Shatt-el-Arab lingesababisha mvutano mkali. Kwa sasa lakini si Iran wala Uingereza ambayo ina maslahi yoyote ya kuanza mzozo wa kijeshi.

Kwa hivyo mzozo huu unapaswa kutatuliwa kwa kutumia diplomasia pekee. Lakini haya ni rahisi kusema kuliko kuyafanya. Kabla ya waziri mkuu Tony Blair kung'oka madarakani lazima awaonyeshe Waingereza kuwa yuko tayari kulinda raia wake.

Kwa upande wa Iran vile vile mzozo huu unaifaa, kwani bila ya kujali ikiwa tukio hili limepangwa awali au la, ni fursa nzuri kuilipiza kisasi Uingereza baada ya kuwekewa vikwazo zaidi.

Kuonyesha video ile ya setilaiti ambayo lengo lake ni kutoa ushahidi kuwa wanamaji hawa walikuwa katika bahari ya Iraq wakati waliposhikwa na Wairan haitasaidia kupunguza ukali wa mzozo huu. Yule ambaye hataki kuamini picha hizo, hataziamini. Iran haitaki kuziamini. Na juu ya hayo, ushahidi huo hauna thamani kubwa kwa sababu mipaka katika eneo hili ni jambo ambalo limezusha mivutano mingi kwa muda mrefu sasa.

Basi, katika hali kama hii, serikali ya Uingereza haina machaguo mengi. Pengine lakini ingefaa zaidi kutokasirishwa na kulizungumzia tukio hili kama kosa lililofanywa kwa bahati mbaya badala ya kubaki kwenye msimamo mkali. Lakini msemo huo wa Kijerumani, mwenye akili zaidi atakubali kushindwa, msemo huo ni mkakati wa nchi zinazoendesha vita. Hapa lakini mkakati huo ungesaidia kupunguza makali. Ikiwa Teheran ingebaki kwenye msimamo wake, na pale tu, Uingereza ingeshindwa. Sasa lakini serikali ya Blair imeingia katika mzozo ambao haiwezi kushinda, na haya yote yataleta athari zaidi kwa wanamaji hawa 15.