Francois Hollande kuzuru Chad leo
18 Julai 2014Ziara hiyo inakosolewa kama anavyokosolewa Deby binafsi, ambaye aliingia madarakani mwaka 1990 kupitia mapinduzi ya kijeshi na hadi sasa nchi hiyo imeshuhudia demokrasia finyu kabisa. Wakati anaunga mkono juhudi za Ufaransa na Umoja wa Mataifa kutatua mizozo ya kimkoa kwa kutumia jeshi lake lenye vifaa vya kisasa, kama alivyofanya nchini Mali, nchini mwake huwachukulia hatua kali wakosoaji wake.
Wachunguzi wa masuala ya kisiasa wanasema kupitia jeshi lake ameweza ameimarisha nguvu zake madarakani.
Idriss Deby ametumia fedha zinazotokana na mauzo ya mafuta nchini mwake kujenga jeshi lake pamoja na sera za mambo ya kigeni, anasema Helga Dickow, mtaalamu wa masuala ya Chad kutoka taasisi ya Arnold-Bergstraesser katika chuo kikuu cha mjini Freiburg nchini Ujerumani, alipokuwa akizungumza na Deutsche Welle.
Utawala wa mkono wa chuma
Sera zake za mambo ya ndani zimemsaidia kujenga uwezo wake wa madarakani ya kisiasa. Deby amewafanya baadhi ya watu kumuunga mkono na kuwatumia. Kati ya hao wamo baadhi ya wapinzani wake wa kisiasa ambao amewanyamazisha , wengine akiwapa nyadhifa muhimu katika mfumo wake wa uongozi. Yule atakayekataa , hufuatwa.
Ukaribu huu wa Ufaransa na Chad, sio mpya. Ufaransa ambayo ni mkoloni wa zamani wa Chad imekuwa hivyo wakati wote. Mwaka 1990 , ilimsaidia Deby kumwangusha kutoka madarakani mtamgulizi wake Hissene Habre. Mwaka 2008 Ufaransa ilikuwa tayari kumsaidia Deby , wakati waasi walipotaka kumtoa madarakani.
Kwa hiyo kwa Ufaransa nchi hiyo ya Afrika ya kati sio tu ni muhimu kiuchumi, lakini pia kimkakati anaeleza mtaalamu wa uhusiano kati ya Ufaransa na Afrika Antoine Glaser.
"Siasa ya Ufaransa kuelekea bara la Afrika hivi sasa, sio hasa inaamuliwa na wanadiplomasia, lakini ni wanajeshi, kwa zingatio la mikakati ya kijiografia, bila kutoa uzito kwa haki za binadamu."
Mapambano dhidi ya ugaidi
Katika mji mkuu N'Djamena na katika mji wa Abeche upande wa mashariki vikosi vya jeshi la Ufaransa vinashikilia maeneo mawili muhimu.
Kituo cha jeshi mjini N'Djamena kina umuhimu mkubwa . Katika kituo hicho kutakuwa na kikosi kipya kitakachoweza kuvuka mipaka na kuchukua hatua kupambana na makundi ya kigaidi kwa ajili ya bara la Afrika , kikosi ambacho kimetolewa mwito wa kuanzishwa na Ufaransa.
Kikosi hicho kitakachojulikana kama operesheni "Barkhane" ama nusu mwezi , kitachukua nafasi ya operesheni ya hivi sasa ya "Serval", ambapo wanapambana na makundi ya wapiganaji wa Kiislamu nchini Mali.
Kiasi ya wanajeshi 3,000 wa Ufaransa katika operesheni hiyo Barkhane, watasaidiwa na ndege zisizoruka na rubani , helikopta na ndege za kijeshi , ambapo operesheni hiyo itahakikisha kuanzia katika pembe ya Afrika hadi Guinea-Bissau makundi ya kigaidi ya Kiislamu hayajipanui. Ufaransa pia itaendelea kushirikiana na Mali, Mauritania, Niger, Chad na Burkina Faso.
Kutokana na hali hiyo rais Hollande tangu Alhamis yuko ziarani katika bara la Afrika, na leo atakutana na rais Idriss Deby. Mtaalamu wa mahusiano kati ya Afrika na Ufaransa , Antoine Glaser , amesisitiza wakati wa mahojiano na Deutsche Welle , vipi Ufaransa binafsi imeshtushwa wakati mara baada ya kuingia madarakani Francois Hollande amekuwa akimkumbatia Deby.
Wengi walitarajia , kwamba atakuwa na mahusiano tofauti kuliko ilivyokuwa na mtangulizi wake Nicolas Sarkozy. Wakati Francois Hollande akiwa rais , wanadiplomasia walidhani kuwa hatamkumbatia kabisa Idriss Deby.
Mashirika mengi yanamkosoa Deby na kumtuhumu kuendea kinyume kwa kiasi kikubwa haki za binadamu.
Mwandishi: Köpp , Dirke / ZR / Sekione Kitojo
Mhariri: Josephat Charo