1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

DRC yaahirisha tarehe ya kuzindua chanjo ya AstraZeneca

Daniel Gakuba
14 Machi 2021

Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo imeahirisha kampeni ya chanjo ya AstraZeneca dhidi ya Covid-19, ikifuata mfano wa nchi nyingine kadhaa zilizochukua kama hiyo. Hayo ni kwa mujibu wa taarifa ya serikali ya nchi hiyo.

https://p.dw.com/p/3qbeN
Coronavirus Impfstoff Symbolbid
Picha: picture-alliance/Flashpic

Serikali ya nchi hiyo ilipokea dozi milioni 1.7 ya chanjo hiyo inayotengenezwa na kampuni ya AstraZeneca ya Uingereza na Sweden, na ilitarajiwa kuanza zoezi la kuwachanja watu Jumatatu ya tarehe 15 Machi.

Soma zaidi: Chanjo ya Covid 19 yawasili Kinshasa

''Tumeamua kuchelewesha tarehe ya uzinduzi wa chanjo hii nchini Kongo, kama hatua ya tahadhari.'' Ameeleza waziri wa afya Eteni Longondo katika taarifa iliyotolewa mjini Kinshasa.

Denmark, Norway, Bulgaria na Iceland zilisimamisha matumizi ya chanjo ya AstraZeneca wiki hii, kama hatua ya tahadhari kufuatia hofu kuwa huenda ilikuwa ikisababisha kuganda kwa damu miongoni mwa watu walioipokea. India kwa upande mwingine ilitangaza Jumamosi, kwamba inaanzisha uchunguzi wa kina kujua athari za baada ya chanjo dhidi ya Covid-19.

WHO yasema chanjo ni salama

Hata hivyo, Shirika la Afya Ulimwenguni, WHO limesema hakuna uhusiano wowote kati ya chanjo ya AstraZeneca na kuganda kwa damu, na limesisitza kuwa chanjo hiyo ni salama.

''Ndiyo, tunapaswa kuendelea kuitumia chanjo ya AstraZeneca,'' amesema msemaji wa WHO Margaret Harris, akiongeza lakini kuwa wasiwasi wowote wa usalama wa chanjo hiyo lazina ufanyiwe uchunguzi.

DR Kongo Eteni Longondo Gesundheitsminister
Eteni Longondo, Waziri wa Afya wa DRCPicha: Imago Images/Tass/D. Feoktistov

Kampuni ya AstraZeneca nayo imekanusha madai dhidi ya chanjo yake ikisema hakuna uhahidi wowote kuwa wanaoipokea wanakabiliwa na hatari ya kuganda kwa damu.

Soma zaidiWHO yahimiza tahadhari juu ya Ebola, Guinea na DRC

Huko Kinshansa waziri wa Afya amesema tarehe mpya ya kuanzisha kamoeni ya chanjo itatangazwa baada ya kupata majibu ya uchunguzi utakaofanywa na wataaamu wa kitaifa na wa kimataifa.

Visa vipya vitatu vyagunduliwa Norway

Maafisa wa afya nchini Norway wamesema visa vitatu vya kuganda kwa damu na kuvuja damu katika ubongo vimeripotiwa miongoni mwa watu wa umri mdogo waliopata dozi ya chanjo hiyo ya AstraZeneca, wakiongeza lakini kuwa hawawezi kuthibitisha kuwa matatizo hayo yametokana na na chanjo hiyo.

''Ni jukumu la Kitengo cha Dawa cha Norway kuzichunguza matukio haya yanayodhaniwa kuwa athari za chanjo, na kuchukua hatua muafaka,'' amesema Geir Bukholm, Mkurugenzi wa Taasisi ya Norway ya Afya ya Jamii anayehusika na kudhibiti magonjwa ya kuambukiza.

Msemaji wa kampuni ya AstraZeneca ameliambia shirika la habari la AFP, kwamba ''usalama wa chanjo (yao) umethibitishwa na utafiti wa kina wa ngazi ya tatu, na wadau waliolinganisha data zao wamesema bayana kuwa chanjo hiyo inakubaliwa na mwili wa binadamu.''

 

Vyanzo: afp, ap