1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Dortmund ina mtihani dhidi ya Shakhtar

13 Februari 2013

Mabingwa wa soka Ujerumani Borussia Dortmund ni lazima wasahau kichapo walichopata mwishoni mwa wiki iliyopita ili waendelee vyema katika jukwaa la Ulaya watakapomenyana na Shakhtar Donetsk.

https://p.dw.com/p/17dLU
Borussia Dortmund's Jakub Blaszczykowski and Mario Goetze (R) react during the German first division Bundesliga soccer match against Hamburger SV in Dortmund February 9, 2013. REUTERS/Ina Fassbender (GERMANY - Tags: SPORT SOCCER) DFL RULES TO LIMIT THE ONLINE USAGE DURING MATCH TIME TO 15 PICTURES PER GAME. IMAGE SEQUENCES TO SIMULATE VIDEO IS NOT ALLOWED AT ANY TIME. FOR FURTHER QUERIES PLEASE CONTACT DFL DIRECTLY AT + 49 69 650050
Fußball Bundesliga 21. Spieltag Borussia Dortmund Hamburger SVPicha: Reuters

Baada ya kushindwa magoli manne kwa moja nyumbani na SV Hamburg, mkufunzi wa Dortmund, Jurgen Klopp, alikiri kwamba walistahili kushindwa lakini, lazima wafanye merekebisho ili kuepusha matokeo kama hayo hii leo usiku.

Washambuliaji wa Dortmund, Marco Reus na Mario Gotze, wanatarajiwa kuendeleza umahiri wao wa kufunga magoli jinsi walivyong'ara katika awamu ya makundi. Lakini Shaktar walisifiwa sana kutokana na mchezo wao maridadi walipowanyamazisha mabingwa watetezi Chelsea na kuwabandua nje ya kombe hilo msimu huu.

Cristiano kucheza dhidi ya United

Katika kipute kingine, macho yote yataangazwa uwanja wa Santiago Bernabeu wakati wenyeji Real Madrid watakapowakaribisha Manchester United. Mkufunzi wa Madrid, Jose Mourinho, ana matumaini kwamba atakiongoza kikosi chake kwa ushindi wa tatu katika Champions League, lakini anafahamu kitisho kinacholetwa na Manchester United.

Jose Mourinho ana matumaini ya kufuzu katika robo fainali dhidi ya Manchester United
Jose Mourinho ana matumaini ya kufuzu katika robo fainali dhidi ya Manchester UnitedPicha: dapd

Mourinho anasema Real wanataka kushinda kombe hilo la Ulaya kwa mara ya kumi naye anataka kwa mara ya tatu. Anasema hata kama hilo halitafanyika mwaka huu, ataendelea kung'ang'ana hadi mwisho. Wakati Madrid wakiendelea kuyumbayumba katika ligi ya nyumbani, La Liga, United wanapepea katika ligi ya Premier England.

Celtic watokwa jasho

Katika matokeo ya michuano miwili ya jana (12.02.2013) mkufunzi wa Celtic, Neil Lennon, anakiri kwamba timu yake inahitaji muujiza kama ingetaka kugeuza kichapo cha jana nyumbani cha magoli matatu kwa sifuri mikononi mwa Juventus. Waliofungia Juve magoli walikuwa wachezaji Alessandro Matri, Claudio Marchisio na Mirko Vucinic.

Miamba hao wa Italia walionyesha mchezo wa kasi na kufaidika na masihara yaliyofanywa na mabeki wa Celtic. Lennon aliwashangaza mashabiki baada ya kumwanzisha kikosini Efe Ambrose licha ya beki huyo kuichezea Nigeria katika fainali ya kombe la mataifa ya Afrika AFCON ambao waliwashinda Burkina Faso Jumapili iliyopita. Lakini alicheza karata mbaya kwa sababu Ambrose alizembea na kufanya masihara yaliyoikubalia Juve kupata mawili kati ya magoli matatu muhimu ya Juve.

Celtic waliduwazwa katika uwanja wa nyumbani mikononi mwa wageni Juventus mjini Glasgow
Celtic waliduwazwa katika uwanja wa nyumbani mikononi mwa wageni Juventus mjini GlasgowPicha: Reuters

PSG waling'ara

Katika mechi nyingine Paris St Germain iliizidi nguvu Valencia kwa kuifunga magoli mawili kwa moja. Magoli ya PSG yalitiwa kimyani na wachezaji wa Italia, Ezequiel Lavezzi na Javier Pastore, kabla ya beki wa katikati raia wa Ufaransa, Adil Rami, kuifungia Valencia goli la kufuta machozi.

Mshambuliaji wa PSG Zlatan Ibrahimovich hata hivyo alionyeshwa kadi nyekundu katika dakika za mwisho mwisho na hivyo basi ina maana kuwa kikosi hicho cha Carlo Ancelotti kitakosa huduma za nyota huyo raia wa Sweden katika mechi tatu zijazo. Ancelotti amekasirishwa na kadi hiyo huku akisema kwamba ulikuwa uamuzi mkali.

Mwandishi: Bruce Amani/DPA/AFP

Mhariri: Josephat Charo