Darfur - Mgogoro uliosahauliwa
29 Julai 2011Mamlaka ya vikosi vya Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika-UNAMID- kulinda amani katika eneo hilo, yanamalizika mwisho wa mwezi huu Julai, lakini muda wake unatazamiwa kurefushwa. Je, UNAMID imefanikiwa kwa umbali gani huko Darfur? Umoja wa Mataifa unatathmini kuwa kiasi ya watu 300,000 wameuawa na wengine wapatao kama milioni 2.7 wamepoteza makaazi yao katika vita vya wenyewe kwa wenyewe vya miaka minane. Makundi tofauti ya waasi, yanapigana na vikosi vya serikali tangu mwaka 2003 katika eneo hilo la magharibi. Licha ya mikataba kadhaa ya amani kutiwa saini na pande hasimu, hakuna amani iliyopatikana. Katikati ya mwezi huu, makubaliano mapya ya amani yalitiwa saini kati ya serikali ya Sudan na waasi wa Darfur. Afisa wa kitengo cha Afrika cha jumuiya inayoshughulikia umma ulio hatarini, Ulrich Delius anasema:
"Kimsingi, Darfur kuna amani katika karatasi, lakini kwa bahati mbaya, eneo hilo wala halina amani. Watu wanalalamika kuwa wanashindwa kureja katika vijiji vyao vilivyoteketezwa. Hakuna usalama na mara nyingi hushambuliwa katika kambi za wakimbizi."
Wakaazi hao wanalalamika kuhusu ukiukaji wa haki za binadamu. Kwa mfano, waandishi wa habari wanaoripoti kuhusu vitendo vya ubakaji, hushambuliwa. Kwa jumla, ni hali isiyoridhisha - kuna udhalimu mkubwa, hakuna sheria na hakuna amani wala suluhu. Ulrich Delius haamini kuwa amani itapatikana upesi hivyo huko Darfur.
Hata mtaalamu wa masuala ya Sudan, Peter Schumann aliefanya kazi kwa miaka kadhaa na tume ya Umoja wa Mataifa nchini Sudan anasema, hakuna uhakika wa usalama. Huko Darfur, taasisi za serikali zinaelemea zaidi upande wa watesaji kuliko kutekeleza wajibu wa ulinzi. Anakosoa kuwa tangu miaka, imedhihirika kuwa UNAMID haiwezi kutekeleza wajibu wake. Hata hivyo, mtaalamu huyo anaamini kuwa kimsingi, ni busara kwa UNAMID kuwepo huko. Lakini katika suala la kurefushwa mamlaka ya tume hiyo, anasema ni muhimu kuzingatia ufumbuzi wa kisiasa. Hata Ujerumani ambayo mwezi huu wa Julai imeshika wadhifa wa mwenyekiti katika Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, itumie fursa hiyo kushinikiza suluhisho la kisiasa kuhusu Darfur. Hivi sasa, Ujerumani imechangia wanajeshi na polisi wapatao kama kama dazeni moja katika vikosi vya UNAMID.
Mwandishi: Ogunsade,Katrin/ZPR-(P.Martin)
Mhariri Hamidou, Oumilkher