1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Cameroon wafungua AFCON kwa ushindi

10 Januari 2022

Vincent Aboubakar alifunga mabao mawili na kuwapa Cameroon ushindi wa 2-1 dhidi ya Burkina Faso wakati Kombe la Afrika lilipong'oa nanga, baada ya maandalizi yaliyokumbwa na msukosuko wa maambukizi ya virusi vya corona.

https://p.dw.com/p/45Lmk
Fußball Africa Cup of Nations | Kamerun v Burkina Faso
Picha: Kenzo Tribouillard/AFP

Aboubakar alifunga mikwaju miwili ya penalti kunako kipindi cha kwanza baada ya Gustavo Sangare kuufunga goli la kwanza la michuano hiyo na kuwapa uongozi Waburkinabe katika mechi hiyo ya kundi A.

Burkina Faso walipata pigo kabla ya mechi hiyo baada ya kocha wao kamou Malo na wachezaji kadhaa kuambukizwa virusi vya corona hatua iliyopelekea naibu wake Firmin Sanou kuiongoza timu hiyo katika mechi yao ya kwanza.

Mashabiki wa Cameroon wameelezea furaha yao kwa timu yao kupata ushindi wao wa kwanza katika kinyang'anyiro cha mwaka huu katika udongo wa nyumbani.

Fußball Africa Cup of Nations | Kamerun v Burkina Faso
Aboubakar akisherehekea na wachezaji wenzakePicha: MOHAMED ABD EL GHANY/REUTERS

"Ni furaha kwetu kushinda pointi tatu za kwanza. Ni heshima kuu kuandaa mashindano haya baada ya miaka mingi na iwapo Cameroon itashinda tutajivunia sana. Nina furaha isiyo kifani," alisema Ayessi Orelene.

Katika mechi ya pili ya kundi hilo Jumapili Cape Verde walipata ushindi mwembamba wa moja bila walipokuwa wakicheza na Ethiopia ambayo ilipata pigo kwa kuwa kunako kipindi cha kwanza mchezaji wao Yared Bayeh alionyeshwa kadi nyekundu baada ya dakika kumi na mbili tu.