1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Muda wa usitishaji vita kati ya Israel na Hamas kuefushwa?

Angela Mdungu
27 Novemba 2023

Wapatanishi kwenye mzozo kati ya Israel na Hamas wamesema wanakaribia kufikia makubaliano ya kuongeza muda wa kusimamisha mapigano kwa siku nne, ulioanza Ijumaa wiki iliyopita.

https://p.dw.com/p/4ZV0b
Makubaliano | Wafungwa Wakipalestina walioachiwa na mamalaka ya Israel
Wafungwa Wakipalestina walioachiwa na mamalaka ya Israel baada ya makubaliano, wakipeperusha bendera ya Palestina na HamasPicha: Nasser Nasser/AP/picture alliance

Siku hizo nne zinamalizika usiku wa Jumatatu kwa majira ya nchini humo. Misri, Qatar, Marekani, Uhispania na Umoja wa Ulaya zinafanya juhudi za kuongezwa kwa muda huo.

Shirika la habari la AFP, limesema Hamas imewaarifu wasuluhishi kwenye mzozo huo kwamba wako tayari kuongeza muda wa kusimaisha mapigano kwa siku mbili hadi nne.

Soma zaidi: Mapatano kati ya Israel na Hamas yaingia siku ya mwisho

Israel hapo kabla ilisema ingeongeza muda wa kusitisha mapigano kwa sharti la kuachiliwa mateka kumi, kwa kila siku moja ya ziada ya kusimamisha mapigano. Mapema hii leo, msemaji wa serikali ya Israel, Eylon Levy pia alisema kuna uwezekano wa kuongeza muda. Amesema wanataka kupokea mateka wengine 50 baada ya Jumatatu, ili kuwarejesha mateka wote nyumbani.

Mapema viongozi kadhaa wa kimataifa walitoa wito kwa Israel na kundi la Hamas kuongeza muda wa usitishaji vita ili kuruhusu misaada zaidi ya kiutu kuingia katika Ukanda wa Gaza na kuachiliwa kwa mateka wanaozuiwa katika ukanda huo. Wito huo umetolewa wakati viongozi hao wakikutana huko Barcelona nchini Uhispania kujadili mzozo huo.

Borell: Kusitishwa mapigano kutaruhusu misaada Gaza

Katika mkutano huohuo Mkuu wa sera za kigeni wa Umoja wa Ulaya Josep Borrell, pia alisema kuwa anatumai mapigano yatasitishwa kwa muda mrefu zaidi katika Ukanda wa Gaza ili kuifanya hatua hiyo kuwa endelevu wakati kukitafutwa suluhisho la kisiasa.

Diplomasia | Mkuu wa Sera za Kigeni Umoja wa Ulaya Joseph Borrell
Mkuu wa Sera za Kigeni Umoja wa Ulaya Joseph Borrell akizungumza na DWPicha: Dora Diseri/DW

Naye katibu Mkuu wa Jumuiya ya kujihami ya NATO amesema kuwa kurefushwa kwa makubaliano hayo kutaruhusu misaada inayohitajika sana na watu wa Gaza na kuitolea wito Iran kuwadhibiti mawakala wake. Tehran inafahamika kwa kuyaunga mkono makundi yanayoipinga Israel yakiwemo Hamas, Hezbollah na waaasi wa Kihuthi wa Yemen.

Katika hatua nyingine Rais wa Ujerumani, Frank -Walter Steinmeier amesema bunge la nchi yake limetenga kiasi cha dola milioni 7.6 kwa ajili ya kulifanyia ukarabati katika jumba la sanaa la jamii lililoharibiwa na shambulizi la Hamas.

Steinmeier ameitembelea jumuiya ya  Be'eri ambayo ni moja ya jamii zilizoshambuliwa akiwa na rais wa Israel Isaac Herzog  katika shambulio hilo la kushtukiza la Oktoba 7 kusini mwa Israel ambapo watu 1,200 waliuwawa.

Na katika hatua nyingine bilionea na mmiliki wa mtandao wa kijamii wa X Elon Musk, ambaye jukwaa lake hilo limekuwa likituhumiwa kwa matamshi ya chuki dhidi ya Wayahudi hii leo amelitembelea eneo la Israel lililoshambuliwa mwezi uliopita na Hamas, akiambatana na Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu, wakati pia akitarajiwa kukutana na viongozi wakuu nchini humo.

Makubaliano ya kusitisha vita Israel-Hamas kurefushwa?