1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wanajeshi wa AU washambuliwa na makundi ya waasi Somalia

Isabella Mwagodi8 Machi 2007

Wanajeshi wengine mia sita kutoka Uganda wamewasili nchini Somalia licha ya kundi la kwanza la wanajeshi wao,kushambuliwa na makundi ya waasi katika kituo kikuu cha ndege cha Mogadishu Somalia. Wanajeshi hao ni kundi la kwanza la wanajeshi wa amani wa Umoja wa Afrika kuwasili nchini humo,katika juhudi za kukabiliana na hali mbaya ya usalama Somalia.

https://p.dw.com/p/CHIh

Muda tuu kundi la kwanza la vikosi vya wanajeshi mia nne wa AU kutoka Uganda walipowasili nchini Somalia,makundi ya waasi yalitekeleza ahadi yao ya kutowakaribisha kwa kuwashambulia kwa mizinga. Wakati hayo yakijiri, mtu mmoja aliwapiga risasi maafisa wawili wa polisi karibu na kituo kikuu cha ndege cha Mogadishu ambapo wanajeshi hao wa Au wa Uganda wamepiga kambi.

Maafisa hao walipigwa risasi na kuwawa katika kituo cha basi ambapo walikuwa wanalichunga eneo hilo la abiria wanaoingia na kutoka katika kituo hicho cha ndege cha Mogadishu.

Walioshuhudia kisa hicho walisema mshukiwa huyo alitoroka muda tuu alipotekeleza mauaji hayo,maafisa wa polisi wamesema wanamsaka mtu huyo. Visa hivi vinahofiwa kuwa vitazidi,kwa vile kuna makundi mengi ya wapiganaji walioko mafichoni.

Hatahivyo waziri msaidizi wa usalama, Salad Ali Jelle alisema wameimarisha usalama katika kituo cha ndege cha Mogadishu,miripuko hiyo ilikaribisha kundi la kwanza la wanajeshi 370 walipowasili. Uganda imetuma kundi la pili licha ya shambulizi hilo dhihirisho ya azma ya Umoja wa Afrika kuisaidia Somalia.

Wanajeshi hao wa AU wamepelekwa nchini humo kwa madhumuni ya kurejesha amani katika nchi hiyo ambayo imekumbwa na vita kwa zaidi ya miaka 18 sasa. Kundi la kwanza la wanajeshi elfu nane wa Uganda wa umoja wa Afrika,liliwasili mapema wiki hii.Baadhi ya wanajeshi wa Ethiopia waliokuwepo nchini Somalia walianza kuondoka katika makundi madogomaodgo na kushurutisha Umoja wa Afrika kupanga mikakati ya kuongeza wanajeshi,

Visa vya mashambulizi dhidi ya viongozi wa serikali na familia zao vimekithiri tangu Jeshi la Ethiopia liliposaidia kuwaondoa wapiganaji wa muungano wa mahakama za kiislamu mwezi Januari.

Ni wazi kuwa, Wanajeshi wa kulinda amani wa Umoja wa Afrika watawajibika kwanza kujihakikishia usalama wa kutokana na mashambulizi zaidi kutoka kwa makundi ya waasi. Pia wanakabiliwa na changamoto ya kumsaidia rais Abdullahi Yusuf Ahmed aimarishe uongozi nchini kote Somalia.

Hivi majuzi mratibu wa masuala ya haki za binadamu katika umoja wa mataifa Eric Laroch,alisema suluhisho kamili la kuzuia kuzuka kwa migogoro hiyo ni kuwajumuisha katika operesheni za vikosi vya amani ambavyo vinatarajiwa kuwasili nchini humo katika siku za karibuni.

Na viongozi wa jamii mbalimbali za Somali wamteta

kuwa,uongozi wa rais Abdulahi Yusuf unawagawanya raia. Jamii hiyo ya Hawiye ilitoa taarifa yake baada ya shambulizi hilo lililowalenga wanajeshi wa Uganda kutokea.Ugomvi huu baina ya viongozi hao na serikali ya mpito ya Somalia umeonekana pia kama chanzo cha kutokuwepo kwa maelewano baina ya viongozi wa nchi hiyo.

Isabella Mwagodi