Umoja wa Ulaya kusaini mkataba na Serbia
29 Januari 2008Umoja wa Ulaya umeikaribisha Serbia isaini makubaliano ya muda ya kisiasa yatakayoruhusu kuwepo ushirikiano kati ya pande hizo mbili.
Mawaziri wa mashauri ya kigeni wa umoja huo wanaokutana mjini Brussels Ubelgiji, wamesema wangependa kusaini makubaliano hayo tarehe 7 mwezi ujao wa Febrauri, siku nne baada ya uchaguzi wa rais nchini Serbia.
Makubaliano hayo yamefikiwa baada ya Uholanzi kuzuia makubaliano ya kuiandaa Serbia iwe mwanachama wa Umoja wa Ulaya kwa sababu ya serikali ya mjini Belgrade kushindwa kuwakabidhi washukiwa wa uhalifu wa kivita.
Wanadiplomasia wa Ulaya wanaamini kusaini mkataba wa muda wa kibiashara na Serbia kutamsaidia rais Boris Tadic, ambaye anaegemea Ulaya, katika kampeni yake dhidi ya mpinzani wake mkuu Tomislav Nikolic, mwanasiasa mwenye msimamo mkali anayeiunga mkono Urusi.
Swala muhimu linalozungumziwa katika kampeni za uchaguzi nchini Serbia ni hali ya baadaye ya jimbo la Kosovo.