1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaSudan

HRW yasema kundi la RSF lahusika katika ubakaji Darfur

Tatu Karema
17 Agosti 2023

Human Rights Watch, yamesema kuwa kikosi maalum cha wanamgambo wa Rapid Support Forces-RSF na makundi ya wapiganaji shirika nchini Sudan, waliwabaka wanawake kadhaa na wasichana katika mji mkuu wa Darfur Magharibi,

https://p.dw.com/p/4VHmF
Kiongozi wa RSF Luteni Jenerali Mohamed Hamdan Dagalo akiwasalimia wafuasi wake alipowasili kwenye mkutano katika kijiji cha Aprag mnamo Juni 22, 2019
Kiongozi wa RSF - Luteni Jenarali Mohamed Hamdan DagaloPicha: Umit Bektas/REUTERS

Tangu kuanza kwa mzozo wa kivita nchini Sudan kati ya wanajeshi wa Sudan na kikosi cha wanamgambo wa RSF mnamo Aprili 15 Aprili, kikosi hicho na wapiganaji wengine washirika wa Kiarabu wameendesha mashambulizi ya mara kwa mara katika miji na vijiji kwenye jimbo la Darfur Magharibi. Mashambulizi haya yamelenga zaidi maeneo yanayokaliwa na mojawapo ya jamii za watu wasiokuwa wa kabila la Massalit.

Soma pia: Vita Sudan havionyeshi dalili ya kuisha miezi minne baadae

Kikosi cha wanamgambo cha RSF na washirika wake chadaiwa kuhusika katika maasi Darfur

Belkis Wille, mkurugenzi mshirika anayeshughulikia migogoro katika shirika la Human Rights Watch, amesema kuwa kikosi cha RSF na washirika wake, kinaonekana kuhusika na idadi ya visa vya ubakaji na uhalifu mwingine wa kivita wakati wa mashambulizi dhidi ya El Geneina. Wille amesema kuwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa linapaswa kuwaonesha wale waliohusika katika unyanyasaji huo kwamba ulimwengu unatazama kwa kuchukuwa hatua za haraka kukomesha maasi hayo.

Mkurugenzi mtendaji wa shirika la kimatiafa ya kutetea haki za binadamu - Tirana Hassan
Tirana Hassan - Mkurugenzi Mtendaji wa Human Rights WatchPicha: Human Rights Watch

Human Rights Watch yawahoji waathiriwa

Mwishoni mwa nwezi Julai, Human Rights Watch iliwahoji wanawake tisa nchini Chad na msichana mwenye umri wa miaka 15 kutoka El Geneina ambao ni waathiriwa wa ubakaji huo na aina nyingine za unyanyasaji wa kijinsia. 

Soma pia :Jenerali wa juu wa Sudan amshutumu mpinzani wake kwa uhalifu na kuwadanganya raia

Wanne, akiwemo msichana huyo, walibakwa na wanaume wengi. Kulingana na matukio binafsi ya waathiriwa hao na visa walivyoshuhudia, pamoja na maelezo yaliyotolewa na watoa huduma ikiwa ni pamoja na maeneo ambapo matukio hayo yalitokea, Human Rights Watch iliwaorodhesha waathiriwa 78, au walionusurika ubakaji kati ya Aprili 24 na Juni 26.

Makundi ya wavamizi yavalia sare ya RSF

Manusura waliozungumza na shirika hilo la Human Rights Watch, wamesema kuwa kati ya mshambuliaji mmoja hadi sita walitekeleza unyanyasaji wa kijinsia. Vikundi vingi vya wavamizi vilijumuisha wanaume waliovalia sare kamili au zisizo kamili za RSF na baadhi, walivalia nguo za raia. Wakati mwingi, waliwasili kwa kutumia magari yaliokuwa na alama ya RSF. Mwanamke mmoja alimtambua mvamizi wake kuwa mkazi wa Kiarabu wa El Geneina

Soma pia:Mapigano ya Sudan yanazidi kulididimiza taifa hilo

Waliohusika na ubakaji pia wafanya unaynyasaji nwingine

Katika karibu matukio yote yaliyoripotiwa na Human Rights Watch, wale waliohusika na ubakaji pia walifanya unyanyasaji mwingine mkubwa ikiwa ni pamoja na kupiga, mauaji, uporaji, au kuchoma moto nyumba, biashara au majengo ya serikali. Watu wote walionusurika wanasema kwamba washambuliaji hao walitaja makabila yao na kutumia matusi ya kikabila kuhusu Wamassalit au wasio Waarabu.

Mzozo wa wakimbizi wa Sudan

Sheria ya kimataifa ya kibinadamu, inayoitwa sheria ya vita, inakataza wahusika kwenye mzozo wa kivita kuwadhuru raia kwa makusudi. Kifungu cha 3 katika Makubaliano ya Geneva ya 1949 na sheria ya kimataifa ya kitamaduni kuhusu haki za binadamu ambazo zote zinatumika kwa pande zote zinazopigana nchini Sudan, zinakataza ubakaji na aina zingine za unyanyasaji wa kijinsia.