1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroUkraine

Zelensky ataka NATO kujadili ulinzi wa anga wa Ukraine

Bruce Amani
17 Aprili 2024

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky amesema mjini Kiev kuwa anapanga kuitisha mkutano wa Baraza la Jumuiya ya Kujihami NATO na Ukraine ili kutoa wito wa kuimarishwa ulinzi wa anga ya nchi yake.

https://p.dw.com/p/4erkE
Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky
Ukraine inataka Baraza la NATO-Ukraine kujadili uimarishwaji wa anga ya nchi hiyo kutokana na kitisho cha mashambuliziPicha: Gints Ivuskans/AFP

Akilinganisha hali ya Ukraine na ile ya Israel, baada ya shambulizi kubwa la Iran la makombora na droni kuzuiwa mwishoni mwa wiki, Zelensky amesema Ukraine itaomba kupewa mifumo ya ulinzi wa mashambulizi ya angani na makombora. Amesema Waukraine wana haki ya kulindwa dhidi ya ugaidi.

Rais huyo wa Ukraine alimpongeza Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz kwa kutafuta suluhisho la mzozo huo. Akizungumza na Rais wa China Xi Jinping mjini Beijing jana, Scholz alisisitiza umuhimu wa China kwenye jukwaa la kimataifa. Kama mshirika muhimu wa Urusi, Xi anaonekana kuwa na ushawishi kwa Rais wa Urusi Vladmir Putin.

Zelensky amesema China inaweza kusaidia kurejesha amani nchini Ukraine na utulivu katika uhusiano wa kimataifa. Uswisi itakuwa mwenyeji wa mkutano wa kilele wa amani katikati ya mwezi Juni, ambao China imealikwa na wala sio Urusi.