Wahariri wa magazeti ya Ujerumani
21 Desemba 2010Wahariri wa magazeti ya hapa Ujerumani wamejishughulisha zaidi hii leo na hali baada ya uchaguzi huko Belarus, ziara ya waziri mkuu wa jimbo la Bavaria nchini Ujerumani Horst Seehofer huko jamhuri ya Czech , na pia barafu nyingi inayoanguka katika bara la Ulaya na kusababisha kuvurugika kwa safari.
Tukianza na hali huko nchini Belarus, gazeti la Nordwest Zeitung la Oldenburg linaandika.
Iwapo Urusi haitaacha kuyanyooshea kidole mataifa ya magharibi kutokana na shutuma zake, hali haitabadilika. Rais wa Belarus Lukashenko anaendelea kuwa na uhuru wa kufanya atakavyo licha ya miito, vitisho na pia kuzuiwa kusafiri katika mataifa ya umoja wa Ulaya. Ni watu wa Belarus pekee ambao wanaweza kubadilisha hali hiyo. Umoja wa Ulaya unaweza tu kutoa msaada wa kiutu. Lakini hali bado inaonekana kuwa ni mbaya. Matamshi ya Lukashenko kwamba wapinzani watashughulikiwa kwa nguvu zaidi, hayaleti matumaini kabisa.
Gazeti la Sächsische Zeitung la mjini Dresden likizungumzia kuhusu mada hiyo linaandika.
Lukashenko anaendelea kufanya kile atakacho. Kwa kuwakamata watu kadha pamoja na kuwashambulia waandamanaji ambao wanapinga matokeo ya uchaguzi wa rais , ameendelea kusherehekea ushindi wa kuchaguliwa kwake. Hakuna jipya kwa hiyo kutoka Minsk mji mkuu wa Belarus, na kila mmoja angeshangaa iwapo kungekuwa na jipya.
Mhariri wa gazeti la Rhein - Neckar-Zeitung la mjini Heidelberg anazungumzia ziara ya waziri mkuu wa jimbo la Bavaria nchini Ujerumani huko jamhuri ya Czech. Gazeti linaandika.
Horst Seehofer na mwenzake wa jamhuri ya Czech Petr Necas wamezungumzia pia masuala kadha ya kisiasa katika mkutano wao mjini Prag, pamoja na masuala ya kiuchumi, kitamaduni na pamoja na mambo kadha mengine ya kawaida. Mzozo kuhusu suala la kufukuzwa Wajerumani waliokuwa wakiishi nchini humo hata hivyo halijatatuliwa. Suala hilo hata hivyo limetupwa nje ya mjadala. Hali ya kuongeza ushirikiano ni njia ambayo inatumika hapa kuondoa hali ya kutoweza kuzungumzia chochote kilichotokea katika wakati baada ya vita.
Kufukuzwa kwa Wajerumani waliokuwa wakiishi katika ardhi ya jamhuri ya Czech na mauaji ni suala ambalo ni tata, na wanasiasa wa nchi hiyo wanatetea hatua hiyo kuwa ilikuwa ni lazima wakati huo, lakini hata Seehofer anataka kuchukua mtazamo mwingine wa ushirikiano kama mtaji kati ya nchi hizi mbili.
Gazeti la Märkische Oderzeitung la mjini Frankfurt -Oder linazungumzia kuhusu hali ya mtafaruku iliyosababishwa na kuanguka kwa theluji nyingi barani Ulaya hivi sasa. Gazeti linaandika.
Kila mwaka hali ni ile ile, wanasema maafisa na makampuni. Tuko tayari kwa majira ya baridi. Huo ni wakati ambao hakuna barafu. Mara baada ya kuanza kuanguka barafu, hayo huyasikii tena wala kuyaona. Mara hii tumejifunza zaidi kutoka kwa kampuni ya treni. Nyakati za majira ya baridi ni wakati ambao wasafiri na wale wanaotaka kwenda likizo wanajitayarisha kwa matatizo. Lakini kama walipa kodi na wateja wanaona kuwa majigambo ya wakati wa majira ya mapukutiko kwamba wako tayari kwa majira ya baridi ni maneno matupu ambayo yameishia kuganda wakati huu wa baridi kali.
Mwandishi : Sekione Kitojo / Inlandspresse
Mhariri: Abdul-Rahman