1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uturuki na uhuru wa vyombo vya habari

25 Machi 2007

Umoja wa Ulaya,mwanzoni mwa Oktoba mwaka 2005,ulifungua rasmi majadiliano kuhusika na ombi la Uturuki la kutaka kuwa mwanachama katika umoja huo.

https://p.dw.com/p/CHHa

Lakini mara kwa mara,Uturuki imekosolewa na Brussels kuwa haikufanya mageuzi ya kutosha upande wa haki za binadamu na uhuru wa maoni.

Kwa mujibu wa “Maripota wasio na Mipaka”-shirika lisilo la kiserikali,zaidi ya waandishi 20 wanakabiliwa na mashtaka ya uhalifu nchini Uturuki.Wengi wao wameshtakiwa kuhusika na kipengele cha sheria kinachosema,kitendo cha kufedhehesha Uturuki ni kosa la uhalifu.Kwa sababu hiyo,baadhi ya vyombo vya habari vinajizuia kuripoti juu ya mada fulani.Kwa upande mwingine,wapo waandishi wanaoeleza waziwazi mada nyeti,kama vile ukiukaji wa haki za binadamu, mashambulio dhidi ya Wakurd,ubakaji na dhima ya jeshi nchini humo.Kwa mfano Tolga Korkut ambae ni mwandishi wa habari wa jukwaa la mtandao “Bianet” amesema,hapo zamani alipofanya kazi kwenye vyombo mbali mbali vya habari nchini humo, alihisi kuwa anachunguzwa kile anachoandika, lakini sasa katika shirika la “Bianet” mambo ni tofauti kabisa kwa sababu anaweza kufanya kazi yake kama ipasavyo.

Masuala yanayohusika na haki za binadamu ni fani kuu ya Korkut-mada ambayo ni nyeti kabisa nchini Uturuki.Na shirika la “Bianet” linajishughulisha sana na mada za eneo la Kusini-Mashariki ya nchi wanakoishi Wakurd wengi.Hali ya eneo hilo na hasa ile ya wanawake wa Kikurd bado ni ngumu sana. Kwani katika eneo hilo ambalo ni masikini kabisa nchini Uturuki,mila na tamaduni zimetia mizizi. Vile vile majeshi ya Uturuki kwa sehemu fulani huchukua hatua kali katika eneo hilo.Mara kwa mara,sehemu hizo kuna vitendo vya adhabu,ubakaji na mateso.Na ni hatari kwa waandishi wa habari kuripoti kuripoti juu ya vitendo hivyo.Hata anaeandika kuhusu chama cha Wakurd cha PKK kilichopigwa marufuku,hujitia hatarini.Kwa mfano, Ragip Duran alifungwa jela miezi 10,kwa sababu ya kuchapisha mahojiano aliyofanya na kiongozi wa PKK-Abdulla Öcalan hapo mwaka 1994.Mahojiano hayo yalichapishwa katika gazeti linalowaunga mkono Wakurd.Sababu iliyotolewa na Mahakama ya Usalama wa Taifa ni kwamba Duran kwa kuchapisha mahojiano hayo,alikifanyia propaganda chama cha ugaidi.

Juu ya hivyo,Duran anasema,katika miaka ya hivi karibuni kumefanywa mageuzi mengi yalio mazuri. Lakini serikali kwa kupitisha sheria fulani tu, haitoweza kuondosha vikwazo vinavyochelewesha uanachama wa Uturuki katika Umoja wa Ulaya. Anasema,utaratibu wa kubadilisha fikra za binadamu huchukua muda.Na hapo ndio yeye pia angependa kutoa mchango wake kupitia “Bianet” kwani mara kwa mara hutoa mafunzo kwa waandishi wa habari vijana.Mbali na kuwapa ujuzi wa uandishi habari,lengo lake kuu ni kuwapa hisia za kuweza kujiamini kwani ni vugumu sana kuwa mwandishi wa habari nchini Uturuki na hasa katika eneo la Wakurd.