Urusi na Umoja wa ulaya
4 Januari 2009Berlin:
Urusi inataka kufikia makubaliano ya ushirikiano pamoja na Umoja wa ulaya mnamo mwaka huu wa 2009.Hayo ni kwa mujibu wa balozi wa Urusi nchini Ujerumani.Akizungumza mjini Berlin,balozi Wladimir Kotenew amesema Umoja wa ulaya umejitokeza kua mpatanishi hodari na mwenye bidii katika mzozo wa Caucasus kati ya Urusi na Georgia.Mwenyekiti wa zamani wa umoja wa ulaya,rais Nicolas Sarkozy wa Ufaransa,amefanikiwa kuzuwia hali ya mambo isizidi kuharibika-amesema balozi huyo wa Urusi mjini Berlin.Bwana Wladimir Kotenew ameikosoa hata hivyo jumuia ya kujihami ya magharibi kwa kushindwa kuushughulikia ipasavyo mzozo huo Agosti mwaka jana.Mwanadiplomasia huyo wa Urusi ameongeza kusema ufumbuzi wa muda mrefu wa mzozo wa Caucasus utawezekana tuu ikiwa serikali mpya itaingia madarakani mjini Tiflis.