Ureno yapeta, Ufaransa hoi
16 Novemba 2013Alikuwa Cristiano Ronaldo maarufu kama CR7 ambaye alikuwa shujaa wa Ureno jana usiku wakati alipopachika bao la kichwa ambalo linaiweka timu ya taifa hilo katika nafasi nzuri ya kukata tikiti yake katika fainali za kombe la dunia mwakani nchini Brazil, baada ya kuishinda Sweden kwa bao 1-0.
Hili ni pigo la binafsi alilotoa Ronaldo kwa Zlatan Ibrahimovic katika mpambano kati ya nyota hao, ambapo mmoja wao atabakia nyumbani wakati wa tamasha la soka kule Brazil mwakani. Hadi alipopachika bao hilo, Ronaldo alikuwa akisumbuliwa mno na ukuta mgumu wa Sweden , alipoteza mikwaju miwili kwa kubamiza mipira katika ukuta huo wa walinzi wa Sweden na alipewa kadi muda mfupi kabla ya bao lake kwa kumfanyia rafu mlinda mlango wa Sweden Andreas Isaksson na fadhaa yake ilipanda zaidi.
Sweden ilipata nafasi kadha katika kipindi cha kwanza kabla ya Ureno kuchukua udhibiti wa mchezo huo baada ya mapumziko, na kupata nafasi ya uongozi katika mchezo wa duru ya pili utakaofanyika hapo Jumanne ijayo.
Ufaransa yageuka kichwa cha mwendawazimu
Wakati Ureno ikijiwinda kuelekea Brazil mwakani , kigogo cha soka barani Ulaya Ufaransa kiko katika hatari ya kuwa mtazamaji , baada ya kuadhiriwa na Ukraine kwa kufungwa mabao 2-0 katika mchezo wa kwanza hapo jana . Iceland ikiwa na wachezaji 10 uwanjani ilipambana na kufanikiwa kutoka sare ya bila kufungana dhidi ya Croatia mjini Reykjavic na kuweka matumaini yake hai ya kuweza kufuzu kucheza katika fainali muhimu za kimataifa kwa mara ya kwanza , wakati Ugiriki ikitoka kifua mbele dhidi ya Romania kwa kuichapa mabao 3-1 mjini Athens.
Miongoni mwa timu nane za bara la Ulaya ambazo zinawania fursa ya mwisho baada ya kushindwa kupata tikiti ya moja kwa moja kuelekea Brazil , Ufaransa iko katika hali mbaya zaidi wakati wakiingia katika mchezo wa mwisho wiki ijayo baada ya usiku mbaya kabisa mjini Kiev jana.
Magoli ya kipindi cha pili yaliyowekwa wavuni na Roman Zozulia na Andriy Yarmolenko pamoja na kadi nyekundu dhidi ya mlinzi wa Ufaransa Laurent Koscielny yalifanya kuwa usiku wa kustahili kusahaulika kwa kikosi hicho cha kocha Didier Deschamps , ambacho kinahitaji uhai wa kutosha mjini Paris siku ya Jumanne ili kufanyia ukarabati madhara hayo yaliyotokea.
Lakini kocha Didier Deschamps amesema kuwa kikosi chake kina nafasi ya kufuzu katika mchezo wa mwisho hapo Jumanne , licha ya kukiri kuwa kikosi chake kilishindwa kuhimili vishindo vya wapinzani wao Ukraine na kukubali kipigo hicho cha mabao 2-0.
Mbali ya michuano hiyo ya kuwania kufuzu kucheza katika fainali za kombe la dunia mwakani, lakini pia kulikuwa na mapambano ya kirafiki katika bara la Ulaya na kwingineko. Italia timu inayoipa Ujerumani ndoto za jinamizi kila mara imethibitisha kuwa haina nafasi ya kuiachia Ujerumani kutamba mahali popote baada ya jana kutoka sare ya bao 1-1 katika mchezo wa kirafiki mjini Milan. Ujerumani ilishindwa kufurukuta dhidi ya mahasimu wao hao jana katika mchezo ambapo kocha Joachim Loew alisherehekea mchezo wake wa 100 tangu kuchukua uongozi wa kikosi hicho.
Chile mwiba kwa Uingereza
Uingereza ambayo inacheza na Ujerumani katika mchezo mwingine wa kirafiki wiki ijayo, ilijikuta ikisalimu amri mbele ya Chile ambayo ilikuwa mwiba mbele ya vigogo hao wa soka katika bara la Ulaya. Kocha wa Uingereza Roy Hodgson ameapa kuwa atarejesha kikosi chake cha kwanza kwa ajili ya mchezo wa Jumanne dhidi ya Ujerumani baada ya kukiona kikosi chake kisicho na uzoefu kikipokea kipigo cha mabao 2-0 dhidi ya Chile.
Michezo mingine ya kirafiki ilikuwa Korea ya kusini ilichapa Uswisi kwa mabao 2-1, Urusi ikatoka sare ya bao 1-1 dhidi ya Serbia, Jamhuri ya Ireland ikaichapa Latvia kwa mabao 3-0. Swaziland ilikubali kipigo cha mabao 3-0 dhidi ya Afrika kusini na Belarus ikatoka sare ya bila kufungana na Albania.
Huko barani Afrika, Mabingwa wa Afrika Nigeria wanatarajiwa kujihakikishia nafasi yao katika dimba la Kombe la Dunia mwakani , lakini Cameroon na Cote d'Ivoire wanakabiliwa na mtihani mkubwa dhidi ya Tunisia na Senegal. Nigeria wanacheza leo Jumamosi katika mchuano wa mkondo wa pili dhidi ya Ethiopia wakiwa na faida ya magoli mawili kwa moja kutokana na mechi ya mkondo wa kwanza iliyochezwa mjini Addis Ababa. Cameroon na Tunisia zilitoka sare ya kutofungana bao mjini Tunis, nayo Cote d'Ivoire ikaizaba Senegal tatu kwa moja nyumbani.
Mwandishi: Bruce Amani/Sekione Kitojo/ AFP/reuters
Mhariri: Josephat Charo