1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yatoa darasa gani la kuvumiliana ?

14 Oktoba 2009

Ni moja ya mada zinazochambuliwa na wahariri:

https://p.dw.com/p/K62Y

Maoni ya wahariri wa magazeti ya Ujerumani leo, yamegusia mada mbali mbali kuanzia siasa za ndani ya nchi-kutoka juhudi za kuunda serikali ya muungano mjini Berlin kati ya vyama vya CDU/CSU na FDP, na sera za kodi hadi dai la sehemu ya Jamii ya waislamu kuwa watoto wao waruhusiwe wasiende mashuleni wanapoadhimisha siku kuu za kiislamu kama Idd.

"Ujerumani ni nchi ya uvumilivu,kwani pembezoni mwa makanisa ,misikiti yaruhusiwa. Katika maktaba huwapo pia kitabu kitakatifu cha koran pembezoni na biblia. Mahkama imetoa hukumu kuwa watoto wa kiislamu waruhusiwe kusali mashuleni bila kero .Juu ya hivyo, wakristu na waislamu wana mengi ya kujifunza:

Katika kujifunza huko, ni kuthubutu kuuliza maswali.Kwa mfano, kwanini ni mwiko katika nchi za kiislamu kujenga makanisa na ni mwiko kufanya ibada za kikristu ? Kwanini kuwa na biblia kuna adhibiwa vikali ? Kwanini waislamu wanaotaka kubadili dini ili kuwa wakristu hutishiwa kifo ? "

Kwa hivyo, linaongeza gazeti la BILD, kuna mengi ya kujifunza .Kwa mfano , kila mmoja popote alipo , aruhusiwe kuabudu Mungu amtakae, kila dini iheshimu dini ya mwenziwe.Darasa hilo la kujifunza linaitwa "kuvumiliana". Na darasa hilo wengi waweza kujifunza kutoka Ujerumani. Na sio tu katika siku kuu za Iddi.

Hilo lilikuwa BILD Zeitung.

Ama kuhusu juhudi za kuunda serikali ya muungano ya Ujerumani mjini Berlin, gazeti la WESTFÄLISCHE NACHRICHTEN laandika:

"Chama cha FDP kiko njia panda na hikijui kifuate ipi? Ni sawa tu kwa Kanzela Angela Merkel ikiwa Kiongozi wa FDP Bw.Westerwelle anapunguzwa makali na hali ya mambo ilivyo.Kinachowezekana na kisichowezekanma, kitaamuliwa na taarifa zijazo za hali ya uchumi.

Serikali ya Ujerumani , imeamua kutangaza na mapema ijumaa hii makisio yake ya mkondo wa uchumi utakavyokua tena kabla vyama hivyo vya CDU/CSU na FDP kukutana kwa kikao chao kikuu . Uchumi utapungua mwaka huu kwa kima cha 4.5 % badala ya 6 % kinyume na ilivyokisiwa kabla. Minon'gono yasema hivyo huko Berlin.Kwa vyama vya muungano vya CDU/CSU vyaweza kumudu hali hiyo ,kwa chama cha kiliberali cha FDP,kima hicho hakitoshi kuchupa mbali usoni."

Gazeti la Sächsische Zeitung linalochapishwa Dresden, linachambua sera za utozaji kodi likandika:

"Ni sawa, laona gazeti -shabaha ya kuwapunguzia raia mzigo wa kodi na hasa familia za wanyonge pamoja na nyongeza za mishahara kuona ni za wastani."

Gazeti laongeza:

"Hakuna mtu mwenye busara atakaepinga mageuzi ya aina hiyo.Kupunguza mno kodi, fedha ziliopo hazitoshi.Na kufanya mageuzi kama kitakavyo chama cha FDP,itakuwa taabu kutimiza shabaha hiyo kinyume na vyama hivi vinavyounda serikali ya muungano, vinavyodhani."

Mwishoe, gazeti la Nüremberger Zeitung lazungumzia maionesho makuu ya vitabu yanayoendelea mjini Frankfurt ,ambamo China ni mgeni mashuhuri mwaka huu.

Gazeti lakumbusha:

" Mkuu wa maandalio ya maonesho Boos, tayari kabla kufunguliwa , alikosolewa mno.Aliipururia mshipi mno China, kwa kudai maonesho haya ni kuipigia debe tu China na vitabu vyake. Lakini, kuna sauti hazitaridhia kuifanyia China hesani hiyo:Frankfurt zitasikika pia sauti za wakereketwa wa upande wa upinzani,zile za watungaji-mashairi wanaoishi nje ya China .Kwahivyo, mambo yatasisimua kwenye burdani ya uandishi-sanifu.."

Mwandishi: Ramadhan Ali/DPA

Mhariri: Abdul-Rahman