Ujerumani yafunga ubalozi wake wa Moscow, Urusi
7 Agosti 2010Mji mkuu wa Urusi, Moscow, unakabiliwa na moshi kutokana na moto mkubwa ambao umekuwa ukiwaka katika maeneo mbalimbali nchini humo tangu wiki iliyopita. Ndege zilizokuwa zikielekea mjini humo zimeelekezwa kutua katika viwanja vingine vya ndege kutokana na moshi huo.
Uchafuzi wa hewa mjini Moscow umeongezeka mara tano kuliko viwango vya kawaida. Ujerumani imeufunga ubalozi wake mjini Moscow kutokana na moshi huo na kuwaonya raia wake, hususan wenye matatizo ya kupumua na watoto wasiende katika maeneo yaliyoathiriwa.
Moto nchini Urusi unaendelea kuwaka kutokana na upepo mkali na kiwango kikubwa cha joto cha zaidi ya nyuzi za joto 40 katika kipimo cha Celcius. Watu 52 wamekufa nchini Urusi kutokana na moto huo ambao pia unawaka katika nchi jirani ya Ukraine. Serikali imelituma jeshi kuifunga misitu na kuyalinda maeneo ya kuhifadhia silaha.