1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani, Poland na England zajiimarisha

Bruce Amani
27 Machi 2017

Kocha wa timu ya taifa ya Ujerumani Joachim Löw alikamilisha kazi yake baada ya mabingwa hao wa dunia kupata ushindi wa tano kwenye mechi tano katika Kundi lao la kufuzu Kombe la Dunia.

https://p.dw.com/p/2a3tO
Aserbaidschan - Deutschland, 26.03.2017
Picha: picture alliance/dpa/M. Guengoer

Ushindi wao wa 4-1 dhidi ya Azerbaijan mjini Baku ulikuwa suala rahisi tu kwa Wajerumani ambao walifungwa bao lao la kwanza kabisa katika Kundi C. Ujerumani wanaongoza kileleni na pengo la pointi tano dhidi ya Ireland ya Kaskazini ambayo iliizaba Norway 2-0. Nayo Jamhuri ya Czech iliizaba San Marino 6-0. Kocha Löw alielezea kuridhika kwake na matokeo hayo

Kundi F

Fußball WM-Qualifikationsspiel Polen vs. Dänemark in Warschau
Poland wako katika nafasi nzuri ya kufuzuPicha: Reuters/Agencja K. Atys

Uwanjani Wembley, England ilipambana na kupata ushindi wa 2-0 dhidi ya Lithuania. Ni mechi ambayo mshambuliaji Jermain Defoe mwenye umri wa miaka 34 alirejeshwa kikosini na akafunga bao lake la 20 la kimataifa. England sasa imejiimarisha kileleni mwa Kundi F. Vijana hao wa kocha Garry Southgate sasa ndio timu pekee ya Ulaya ambayo haijafungwa bao hata moja kufikia sasa. England wana pointi 13, nne mbele ya Slovakia ambao walisonga katika nafasi ya pili ya kundi hilo kwa kupata ushindi wa 3-1 dhidi ya Malta. Scotland wako nyuma na pengo la pointi sita baada ya kupata ushindi wa 1-0 dhidi ya Slovenia.

Katika Kundi E, nahodha wa Poland Robert Lewandowski alifunga bao katika mechi ya kumi mfululizo na kuiweka kileleni timu yake kwa ushindi wa 2-1 dhidi ya Montenegro. Montenegro sasa iko na pointi saba sawa na Denmark baada ya Wadenmark kutoka sare tasa na Romania, ambayo ina pointi sawa na Armenia. Armenia iliifunga Kazakhstan 2-0 na kuyaweka hai matumaini ya kucheza mechi za mchujo.

Kocha wa uholanzi atimuliwa

Fußball UEFA EURO 2016 Qualifikation Türkei - Niederlande Danny Blind
Danny Blind amepigwa kalamu baada ya kichapo dhidi ya BulgariaPicha: picture-alliance/dpa/T. Bozoglu

Wakati huo huo, Kocha wa Uholanzi Danny Blind ameüigwa kalamu, ikiwa ni chini ya saa 24 tu baada ya kichapo cha 2-0 dhidi ya Bulgaria kuiacha timu yake katika nafasi ya nne ya Kundi A la kufuzu katika dimba la Kombe la Dunia. Shirikisho la kandanda la Uholanzi lilitangaza uamuzi huo kupitia taarifa baada ya Blind, kuitwa kwa ajili ya mazungumzo ya dharura.

Kocha huyo mwenye umri wa miaka 55 amelalamikia uamuzi huo akisema kuwa timu yake ilikuwa kwenye mkondo sahihi na kichapo cha Bulgaria kilikuwa ni pigo. Timu ya taifa ya Uholanzi imekuwa ikiyumba tangu ilipokosa kushiriki dimba la Ubingwa wa Ulaya 2016 hasa ikizingatiwa kuwa miaka miwili kabla, ilimaliza katika nafasi ya tatu kwenye dimba la Kombe la Dunia 2014 nchini Brazil. Jean Paul Decossau ni mkurugenzi wa shirikisho la soka la Uholanzi na hapa anaelezea kilichojiri

Kichapo hicho kimeiacha Uholanzi ikikabiliwa na mtihani mkubwa wa kumaliza katika mojawapo ya nafasi mbili za kwanza za kufuzu katika Kundi A. Ina pointi saba baada ya kucheza mechi tano na wako nyuma ya vinara Ufaransa ambao wana pointi 13, Sweden ina 10 na Bulgaria ina 9. Kocha msaidizi  Fred Grim atachukua usukani katika mchuano wa kirafiki kesho dhidi ya Italia mjini Amsterdam wakati kocha mpya akitafutwa.

Mwandishi: Bruce Amani/AFP/DPA/Reuters
Mhariri: Yusuf Saumu