1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

UHABA WA GESI MATAIFA KADHAA YA BARA LA ULAYA

Jane Nyingi6 Januari 2009

Urusi imesema iko tayari kurejea mashauri na Ukraine kufuatia mzozo kati yao ambao umekatisha

https://p.dw.com/p/GT8j
Mabomba ya gesi nchini UrusiPicha: AP

Urusi hivi leo ilikatisha kabisa usambazaji gesi inayopitia mabomba ya ukraine hatua ambayo imeshtumiwa vikali na umoja wa ulaya.

Mataifa yaliyoathiriwa zaidi ni yale yaliyo mashariki mwa Europa baadhi yao Bulgaria, Romania, Ugiriki,Macedonia na Uturuki ambayo usambazaji gesi ulisimamishwa ghafla kwani hutengemea mambomba ya Ukraine kupata gesi inayotoka katika kiwanda cha uzalishaji gesi asili cha GazProm nchini Urussi.

Umoja wa ulaya umeshtumu vikali hatua hiyo na Urusi na kutaka pande zote mbili kurejelea mashauri ili kutatua mzozo wao wa kibiashara. Tishio hilo la kukatishwa gesi inayopitia mabomba ya ukraine kwenda mataifa ya ulaya kunawadia wakati ambapo msimu wa baridi unaendelea katika mataifa hayo na bidhaa hiyo huhitajika kwa kiwango kikubwa. Kaimu mkurugenzi mkuu wa kiwanda cha Gazprom Alexander Medvedev.

“Licha ya majaribio yote kuileta Ukraine katika meza ya mazungumzo, kwa siku ya tano leo hatujapata mshirika yeyote. Taarifa zote tunapata kupitia vyombo vya habari. Na ni kweli hatuna matumaini yeyote. Japokuwa Gazprom imejitahidi kuhakikisha kuwa gesi inayosambazwa haipungui lakini kampuni hiyo si yenye uwezo wa kipekee. Iwapo Ukraine itaanza kuweka vikwazo na imefanya hivyo kwa kukataa kuongezwa kwa gesi inayosambazwa katika mabomba yake,basi matokeo yake ni ngumu kutabiriwa.”

Ujerumani, Austria na jamuhuri ya Czech pia zimeanza kuhisi athari za mzozo huo kufuatia kupungua kwa kiwango cha gesi inayosafirishwa katika mataifa hayo. Maafisa wa umoja wa ulaya waliokutana na wakurugenzi wakuu wa kampuni ya Gazprom mjini Berlin hapa ujerumani wamesema mataifa mengine ambayo pia yatakayojipata matatani ni Italia ,Hungary, Slovenia na Slovakia.

Jamuhuri ya Czech ambáyo kwa miezi sita itakuwa rais wa muda wa umoja wa ulaya imesema maafisa wa Ukraine wameyahakikishia mataifa yaliyo katika umoja huo, kuwa watajitahidi kuhakisha suluhu linalokubalika linapatikana.

Mkutano mwingine utakaoratibiwa na maafisa wa umoja wa ulaya utafanyika siku ya ijumaa wiki hii ili kutathmini athari ambazo zimetokana na mzozo huo wa Ukraine na Urusi. Wawakilishi kutoka kiwanda kinachozalisha gesi asili nchini Urusi, GazProm na wale wa kampuni ya Naftogaz nchini Ukraine wamealikwa,na pengine huenda ukatumiwa kuanzisha mashauri upya.

Rais wa Ukraine Viktor Yushchenko hata hivyo ameelezea wasiwasi wake kuwa huenda Urussi ikakatisha kabisa usambazaji gesi katika mataifa ya ulaya kupitia Ukraine.Katika taarifa yake rais Yuschenko amesema tayari ameuandikia barua usimamizi wa umoja wa ulaya na mataifa wanachama ambayo yameripoti kiwango cha chini cha gesi.

Urusi ilikatisha usambazaji gesi kwa Ukraine januari mosi kufuatia mzozo wa malipo.Pia iliishtumu Ukraine kwa kuiba gesi ya Urusi iliyonuiwa kwa wateja wake bara la ulaya.