1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ripoti ya taasisi za upelelezi za Marekani kuhusu Irak

Oummilkheir24 Agosti 2007

Hali inatisha ,hata hivyo wanajeshi wa Marekani waendelee kuwajibika

https://p.dw.com/p/CH9B
Picha: AP

Taasisi za upelelezi za Marekani zimechapisha ripoti inayotisha kuhusu hali nchini Irak,udhaifu wa serikali na uhaba wa vikosi vya usalama katika wakati ambapo shinikizo linazidi kukua nchini Marekani,ili iamuliwe kama wanajeshi wao waanze kurejeshwa nyumbani au la.

Ikitangazwa wiki tatu tuu kabla ya matukio matatu muhimu yanayosubiriwa,ripoti hiyo iliyoandaliwa kwa pamoja na taasisi 16 za upelelezi nchini Marekani,inatishia kuwapatia hoja zaidi tangu waungaji mkono mpaka wapinzani wa kuhamishwa wanajeshi wa Marekani toka Irak.

Ikulu ya Marekani-White House inahisi ripoti hiyo inawapa moyo katika kuendeleza mkakati wao.Wakati huo huo lakini ripoti hiyo inamsuta senator mashuhuri wa Republican John Warner aliyedai wanajeshi japo kidogo wanze kurejeshwa nyumbani kuanzia X-Mas.

Kutokana na hasara zilizopindukia tangu za maisha ya binaadam mpaka za fedha zilizosababishwa na vita hivyo na kushindwa serikali ya Irak kuleta suluhu miongoni mwa jamii,wapinzani wa rais Bush toka chama cha Democratic ,wanaodhibiti baraza la Congress na hata marafiki zake wa chama cha Republican wamekua wakimshinikiza aanze kuwahamisha wanajeshi wao.

Hawakufanikiwa mpaka sasa kumlazimisha aandae ratiba.Lakini analazimika kuanzia sasa ajieleze.Hadi kati kati ya mwezi ujao,ikulu ya Marekani inatakiwa iwasilishe ripoti bungeni,inayoangaliwa kua na umuhimu mkubwa.

Ripoti iliyotangazwa jana na taasisi za upelelezi inaonekana kama itaipa nguvu ripoti hiyo ya White House.

“Taasisi za upelelezi zinahisi serikali ya Irak itadhoofika katika kipindi cha miezi 6 hadi 12 ijayo kutokana na lawama zinazotolewa na waumini wa madhehebu ya Shiya,wasunni na wakurd”-wameonya waandalizi wa ripoti hiyo.

“Wakuu wa Irak,wanaoshindwa kutawala ipasavyo,watakua na kazi ngumu ya kuleta suluhu“ ripoti hiyo imeongeza kusema.

Kwa wakati huu tulio nao,ila kama mambo yatabadilika kwa undani kabisa,- hakuna dalili za kupatikana maridhiano ya kisiasa kuimarisha usalama , hakuna ishara ya maendeleo ya kudumu ya kisiasa seuze maendeleo ya kiuchumi.

Ripoti hiyo inazungumzia juu ya maendeleo “yasiyofichika ingawa si ya sawa” katika sekta ya usalama.Lakini inasisitiza pia wanajeshi laki moja na 60 elfu wa Marekani watalazimika kusalia na sio kujiacha nyuma tuu kuwasaidia wanajeshi wa Irak.Hali hiyo itapelekea maendeleo yaliyofikiwa kufifia.

Rais Bush anaweza kuitumia hoja hii ili kupinga madai ya wanaotaka idadi ya wanajeshi wa Marekani nchini Irak ipunguzwe.

Kinyume chake,katika wakati ambapo waziri mkuu El Maliki anazidi kupwaya,wapinzani wa rais Bush wanaweza kuitumia ile hali ya kushindwa wairak kusikilizana,ili kulifikia lengo lao.

“Ripoti imeonyesha kwamba mkakati wetu umepelekea hali ya usalama kuboreka nchini Iraki,ingawa bado changamoto zingalipo-“amesema hayo msemaji wa ikulu ya Marekani Gordon Johndroe.

“Inavunja moyo,japo haistaajabishi kuona kwamba suluhu bado haijapatikana licha ya maendeleo katika sekta ya usalama.”Ripoti imechambua.