PARIS : Mataifa yashindwa kukubaliana juu ya vikwazo kwa Iran
6 Desemba 2006Wanadiplomasia kutoka nchi tano wanachama wa kudumu wa Baraza la Usalama la Umoja wa Maataifa na Ujerumani wameshindwa kukubaliana juu ya rasimu ya azimio kwa ajili ya mpango wa kuiwekea vikwazo Iran kutokana na mpango wake wa nuklea.
Kufuatia mazungumzo yao mjini Paris wizara ya mambo ya nje ya Ufaransa imesema katika taarifa kwamba maendeleo yamefikiwa na kwamba nchi zote husika zimekubali juu ya kupitisha azimio lenye kuweza kufanya kazi ipasavyo.Lakini wanadiplomasia mjini Paris wanasema serikali ya Urusi inapinga kuwekwa kwa vikwazo vikubwa dhidi ya Iran.
Uingereza,China,Ufaransa,Urusi,Marekani na Ujerumani zinachukuwa hatua hiyo kufuatia Iran kupuuza tarehe ya mwisho iliowekwa na Umoja wa Mataifa hapo Augusti 31 kusitisha urutubishaji wa uranium ambao serikali za mataifa ya magharibi zinadai kuwa unaweza kutumiwa kutengeneza silaha za nuklea.
Iran inasisitiza kwamba mpango huo ni kwa ajili ya shughuli za kiraia na Rais wa nchi hiyo Mahmoud Ahmedinejad hapo jana ameyaonya vikali mataifa ya Ulaya kutoingilia kati mpango wake huo na kusema kwamba hatua hiyo inaweza kuhatarisha uhusiano kati ya Iran na Ulaya.