1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

NAIROBI: Mkutano wa kimataifa juu ya mabadiliko ya hali ya hewa watafuta mkataba mpya

7 Novemba 2006
https://p.dw.com/p/CCvE

Mkutano wa kimataifa juu ya mabadiliko ya hali ya hewa ulifunguliwa jana katika mji mkuu wa Kenya, Nairobi. Makamu rais wa Kenya, Moody Awori, ndie aliufungua mkutano huo ambao unagharamiwa na Umoja wa mataifa. Katika hotuba yake, Moody Awori alisema, ongezeko ya joto ni hatari kubwa zaidi kuwahi kuikabili dunia yetu. Kutokana na hali hiyo, Moody Awori, alishauri:

´´Hatunabudi kuzilinda nyenzo zetu. Vinginevyo watu wetu wataendelea kutumbukia katika hali ya umaskini usiokwisha´´.

Ripoti ya Umoja wa mataifa katika mkesha wa mkutano huo, ilisema kuwa madhara ya mabadiliko ya hali ya hewa yameanza kujitokeza katika maeneo kadhaa barani Afrika.

Kwa muda wa wiki mbili, wajumbe kwenye mkutano huo wa mjini Nairobi, wataangalia kwa undani mikakati kuelekea mkataba mpya wa kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa ambao unachukua nafasi ya mkataba wa Kyoto ambao muda wake unamalizika mwaka wa 2012.

Takwim za hivi karibuni ambazo zilitangazwa wiki iliopita, zinasema kiwango cha gesi inaotoka viwandani kimezidi kuongezeka.