Mzozo wa Mashariki ya kati magazetini
19 Novemba 2012Tuanzie lakini mashariki ya kati kwa kuzingatia jinsi wahariri wanavyotathmini hatari inayoweza kuzuka pindi jumuia ya kujihami ya NATO ikiamua kumhami mwanachama wake-Uturuki-dhidi ya hujuma kutoka Syria katika wakati ambapo ugonvi kati ya Israel na Hamas unazidi makali.Gazeti la Kölner Stadt-Anzeiger linaandika
Jumuia ya kujihami ya NATO ingefanya vyema kushinikiza mzozo usizidi makali.Inabidi isaidie kuwazuwia waisrael wasiingie Gaza.Hatua kama hiyo haina umuhimu wowote kijeshi.Kisiasa,vita vya nchi kavu tokea hapo ni vya hatari.Kwasababu vitaifanya Misri ilazimike kuamua.Na itaipa moyo Iran iendelee kupalilia na kwa namna hiyo kuwapunguzia shinikizo washirika wao wa Syria.Waimla wanaofuata nadharia kali katika eneo la mashariki ya kati,wameshaanza kukuna kichwa,wakisubiri lini balaa litaripuka.
Gazeti la Wiesbadener Kurier linatathmini uwezekano wa kutumwa vikosi vya jeshi la Ujerumani, pindi ikilazimika, nchini Uturuki na kuandika:
"Kutumwa wanajeshi wa kigeni ,kama hakuna njia nyengine,kusaidie kuzuwia vita vya wenyewe kwa wenmyewe nchini Syria visienee hadi katika nchi jirani.Hilo ndilo linalobidi kuwa lengo.Ukiangalia jinsi Ufaransa inavyoelemea upande wa upinzani,na kufika hadi ya kutaka kuwapatia silaha,basi hutokosa kutambuwa kwamba mzozo huo wa kimkoa unaweza haraka kuchukua sura ya mzozo wa kimataifa.Kwa namna hiyo kutumwa wanajeshi wa Ujerumani nchini Uturuki hakutamaanisha tena kuihami nchi mwanachama wa jumuia ya kujihami ya NATO.Bunge la Ujerumani,bila ya kujali kanuni za NATO zinasema nini,linabidi lipatiwe nafasi ya kuamua katika suala hilo.
Mada ya pili magazetini inahusu mkutano mkuu wa chama cha upinzani cha walinzi wa mazingira uliomalizika katika mji wa kaskazini wa Hannover kwa kushadidiwa malengo muhimu ya chama hicho.Gazeti la "Neue Presse" la mjini Hannover linaandika:
Katika mkutano wa walinzi wa mazingira,baadhi ya wakati mtu alifikiri anahudhuria mkutano mkuu wa shirikisho la vyama vya wafanyakazi-DGB au ule wa chama cah Social Democrat-SPD,kwa jinsi ilivyohanikiza miito kuhusu "kiwango cha chini cha mshahara" na "mshahara sawa kwa kazi sawa".Miito hiyo inalingana moja kwa moja na ile ya chama cha SPD kwa namna hiyo mtu anaweza kusema walinzi wa mazingira wanaunyemelea uwanja wa wale wanaotaka kushirikiana nao serikalini baada ya uchaguzi mkuu wa mwakani,na sio ule wa serikali ya sasa ya muungano mjini Berlin.Uamuzi uliyopitishwa Hannover lakini unaufanya kuwa muhali muungano wa walinzi wa mazingira na vyama ndugu vya CDU/CSU mjini Berlin.
Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/Inlandspresse
Mhariri:Yusuf Saumu