1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Merkel: Bado vizuizi vya kudhibiti corona vitaendelea kuwepo

Amina Mjahid
26 Novemba 2020

Kansela wa Ujerumani Angela Merkel amesema masharti ya kudhibiti virusi vya corona yataendelea kuwepo kwa mwezi wa Desemba, huku akisisitiza kuwa hatua hizo zimeusaidia mfumo wa afya wa taifa kupambana na janga la corona

https://p.dw.com/p/3lsKd
Berlin | Angela Merkel -  Regierungserklärung zur Bewältigung der Corona-Pandemie
Picha: Kay Nietfeld/dpa/picture alliance

Akilihutubia bunge la Ujerumani, kansela Merkel amewambia wabunge kuwa watu wamepunguza kuonana kwa asilimia 40 kutokana na masharti yaliowekwa yanayoruhusu familia mbili tu kukutana, huku baa, migahawa, na maneno ya kubarizi yakifungwa.

Ujerumani hadi sasa imekwepa kuweka mzigo mkubwa katika mfumo wake wa afya. Merkel amesema wanachokifanya kwa sasa kinafanikiwa, lakini haimaanishi ndio mwisho wa kutafuta mbinu zaidi za kupambana na janga la corona.

Kansela huyo wa Ujerumani ameongeza kuwa bado hawajafikia hatua ya kulegeza masharti hayo kutokana na maambukizi ya virusi vya corona kuwa juu na idadi ya vifo bado ni ya wasiwasi, lakini bado wanafuatilia hali ilivyo.

"Iwapo idadi ya maambukizi itashuka, katika wiki zijazo basi tutatathmini tena hali ilivyo kabla ya krismasi ili tufanye maamuzi mengine, watu wana haki ya kuwa na matarajio yoyote lakini kwa sasa hatuwezi kutoa ahadi ya kulegeza masharti kuelekea krismasi na mwaka mpya ," alisema Merkel

Huku hayo yakiarifiwa baadhi ya viongozi wa majimbo 16 ya Ujerumani wametaka hali hiyo iendelee hadi mwezi Machi mwaka ujao.

Huenda masharti ya kukabiliana na virusi vya corona vikaendelea hadi mwezi Machi

Coronavirus Deutschland Kanzleramtsleiter Helge Braun mit Schutzmaske
Picha: Getty Images/AFP/F. Rumpenhorst

Mnadhimu mkuu wa ofisi ya kansela Merkel, Helge Braun, ameiambia televisheni ya Ujerumani ya RTL kuwa vizuizi vinavyodhibiti mkusanyiko wa watu huenda vikahitajika hadi mwezi wa tatu mwaka ujao.

Helge Braun amesema baada ya muda huo Ujerumani itakuwa imeanza kutoa chanjo kwa watu wengi zaidi na itakuwa rahisi kudhibiti maambukizi ya virusi vya corona. Mikakati iliyowekwa hata hivyo inatarajiwa kuwepo hadi mwanzoni mwa mwaka 2021.

Kwa upande wake kansela Merkel amesema huenda chanjo ya virusi hivyo ikafika Ujerumani kabla ya sherehe za Krismasi na wamekubaliana kuwa chanjo hiyo itatolewa kwa watu wanaofanya kazi katika sekta ya utabibu kutokana na vitisho wanavyokabiliana navyo.

Hadi sasa idadi ya watu waliothibitishwa kuambikizwa virusi vya corona nchini Ujerumani imeongezeka kutoka elfu 22,268 hadi 983,588 hii ikiwa ni kulingana na Taasisi ya udhibiti wa magonjwa ya kuambukiza nchini Ujerumani ya Robert Koch. Vifo vitokanavyo na ugonjwa wa COVID 19 vimeongezeka kutoka 389 hadi elfu 15,160.

Ujerumani ilianza kutekeleza vizuizi vya kudhibiti virusi vya corona Novemba 2 kutokana na wimbi la pili a ugonjwa wa COVID 19 kulikumba bara Ulaya.

Chanzo: dpa/Reuters