Mataifa ya magharibi yapinga mazungumzo zaidi ya Kosovo
13 Desemba 2007NEW YORK
Nchi za magharibi na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa zimepinga shinikizo la Urusi la kutaka kufanyika kwa mazungumzo zaidi juu ya mustakbali wa Kosovo jimbo la Serbia.
Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa Zalmay Khalilzad amesema mchakato wa mazungumzo umetumiwa hadi mwisho kabisa kufuatia kushindwa kwa mazungumzo ya miaka miwili ya kutafuta muafaka kati ya watu wa kabila la Waalbania walio wengi huko Kosovo na Waserbia.
Takriban nchi zote za Umoja wa Ulaya,Marekani na nchi za Kiislam zinasema kwamba kutokana na kushindwa kwa mazungumzo hayo jimbo hilo lililojitenga la Serbia linapaswa kuruhusiwa kujitangazia uhuru.
Serbia na mshirika wake Urusi zinapinga vikali wazo la kupatiwa uhuru kwa jimbo hilo.
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa linajiandaa kuwa na mjadala mkubwa juu ya Kosovo hapo tarehe 19 mwezi wa Desemba.