Maoni ya wahariri juu ya Papa
28 Februari 2013Gazeti la"Neue Osnabrücker linauliza jee ni urithi gani aliouacha Papa Benedikt baada ya kuliongoza kanisa kwa muda wa miaka minane?
Mhariri wa gazeti hilo analijibu swali hilo kwa kueleza kwamba,Baba Mtakatifu huyo anaetokea Ujerumani atakumbukwa kwa kitabu chake juu ya Yesu Kristo,mahubiri yake juu ya upendo wa kanisa na mchango wake katika kuwatetea Wakristo wanaoandamwa katika mabara ya Afrika na Asia. Mhariri wa gazeti la "Neue Osnabrücker "anasema Papa Benedikt wa16 pia atakumbukwa kwa juhudi alizozifanya ili kuudumisha umoja wa Kanisa Katoliki.
Atakumbukwa kwa kuieneza Injili
Mhariri wa gazeti la"Badische"anakumbusha juu ya juhudi za Papa Benedikt za kuliimarisha kanisa.Mhariri huyo anaeleza kwamba Papa Benedikt wa 16 atakumbukwa kwa juhudi za kulieneza neno la Mungu barani Ulaya,ambako watu wengi wamezidi kulipa kanisa kisogo.Lakini juhudi hizo zilihitaji moyo mkubwa sana na siyo tu,kuandika vitabu na nyaadhi.
Gazeti la"Saabrücker" lina maoni tofauti juu ya urithi aliouacha Papa Benedikt. Mhariri wa gazeti hilo anahoji kuwa japo Wajerumani wangelipendelea sana kuyaona mambo vingine,ukweli ni kwamba Baba Mtakatifu huyo, Mjerumani,hakuacha alama kubwa. Yeye ni Baba Mtakatifu ambaye katika historia ya kanisa, atakumbukwa kwa taadhima aliyojijengea kutokana na tabia yake ya unyenyekevu na upendo.Lakini Benedikt wa16, ni Papa alieitumia kidogo sana, fursa iliyokuwapo kuiimarisha imani ya watu ili wasitamauke.
Naye mhariri wa gazeti la "Nürnberger"anasema hatua ya Papa Benedikt wa16 ya kujiuzulu inaweza kuwa ya manufaa makubwa kwa Kanisa Katoliki la barani Afrika linalozidi kustawi,wakati ambapo kanisa hilo linadhoofika barani Ulaya na Marekani.Kutokana na kuweka mkazo katika masuala ya usawa wa kijinsia,uadilifu wa kijinsia na mivutano katika uongozi, wajibu mkuu wa kanisa,ulipuuzwa,yaani kuleta ustawi wa kiroho,na kuuwasilisha ujumbe mtakatifu. Sasa limebakia swali moja muhimu,iwapo, Papa atakaefuatia ataweza kuyatimiza matarijio ya watu ambayo ni ya juu.
Bajeti ya Marekani
Mhariri wa gazeti la"Die Welt"anazungumzia juu ya mzozo wa bajeti nchini Marekani ambako wajumbe wa vyama vya Republican na Demokratik wanaendelea kuvutana Mhariri huyo anatilia maanani kwamba pande mbili hizo zinashindwa kufikia mwafaka juu ya suala hilo.Hata hivyo mhariri huyo anaeleza kuwa ni vizuri kwamba pande mbili hizo zinashindwa kufikia mwafaka .
Sababu ni kwamba kulikata jongoo kwa meno-yaani kukata bajeti halakulihali,kutaleta vilio na machungu katika dola Kuu duniani- Marekani.Hata hivyo,kukata matumizi ni bora kuliko kuifuata njia nyingine,yaani ya kuendelea kuikimbia hali halisi.
Mwandishi: Mtullya Abdu/Deutsche Zeitungen.
Mhariri: Josephat Charo