1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ligi za Ulaya kutimua vumbi

1 Mei 2009

Ligi mbalimbali za kandanda barani Ulaya zinatimua vumbi, ikiwemo Bundesliga, ya Ujerumani.

https://p.dw.com/p/HiFG

Katika ligi hiyo ya Ujerumani Bundesliga, Mabingwa watetezi, Bayern Munich baada ya kumtimua kocha wake Jurgen Klinsmann, leo wanajiwinda kurejesha imani angalau ya kukamata moja kati ya nafasi tatu za juu, itakapokaribishwa na timu inayoelekea kushuka daraja, Borussia Moenchengladbach.

Jupp Heynckes bei Bayern München
Jupp Heynckes kocha mpya wa Bayern Munich.Picha: AP


Bayern itakuwa chini ya kocha wake mpya wa mpito, Jupp Heynckes aliyechukua jukumu la kuinusuru, baada ya Klinsmann jahazi kumuendea mrama.


Mechi hii ya leo utakuwa ni mtihani wa kwanza kwa kocha huyo, dhidi ya timu ambayo ambayo hapo kabla aliwahi kuichezea na pia kuwa kocha wake.


Heynckes akizungumzia jukumu alilobeba alikiri kuwa ni gumu.


CLIP:HEYNCKES

Najua bilashaka kuwa itakuwa ngumu kufanya mabadiliko katika kipindi cha wiki nne.Nadhani hicho ni kipindi kifupi kwa wachezaji kuweza kuwa katika nafasi nzuri ya kujifunza.Timu kama Bayern Munich ni lazima ishiriki katika ligi ya mabingwa ya Ulaya.Na hilo lazima liwe lengo letu pale unapojiandaa kwa mechi ngumu kama hii ya Moenchengladbach.


Kufuzu kwa ligi ya mabingwa Ulaya ni jambo ambalo pia amelisisitizia kiungo wa timu hiyo mfaransa Frank Ribbery.


Ribbery amesema kuwa tiketi hiyo ndiyo kitu pekee kitakachoweza kumzuia kuipa kisogo Bayern Munich, msimu ujayo.Frank Ribbery ameweka wazi hamu yake ya kujiunga na Barcelona ya Uhispania.


Mechi nyingine za Bundesliga hii leo itakuwa ni kati ya vinara wa ligi hiyo Wolfsburg watakaowakaribisha nyumbani Hoffenheim.


Woflsburg inashuka uwanjani huku uvumi ukitanda kuwa kocha wake Felix Magath yuko mbioni kujiunga na Schalker 04.Lakini Magath alitupilia mbali uvumi huo akisema lengo ni ubingwa ambao uko viganjani mwao.


CLIP:MAGATH

Mara zote kama kawaida yangu mimi huwa vitu kama hivi, uvumi na hisia havina nafasi.


Mbali ya pambano hilo kati ya Wolfsburg na Hoffenheim, Schalker 04 watawaalika uwanjani Bayer Leverkusen, huku Karlsruhe wakiwa na kibarua na Cottbus.Frankfurt watakuwa wenyeji wa Borussia Dortmund.


Katika ligi nyingine barani Ulaya, huko Uingereza, Chelsea itaumana na watoto wenzao wa London Fulham, huku Manchester United ikijaribu kujizatiti kileleni itakapokaribishwa ugenini na Middlesbrough.


Mechi nyingine zitakuwa ni kati ya Manchester City na Blackburn Rovers, na Arsenal itapambana na Portsmouth.


Huko Italia Inter Milan itaumana na Lazio, ilhali Bologna watapambana na Reggina.

Mwandishi:Aboubakary Liongo

Mhariri.Mohamed Abdul-Rahman