Kansela Merkel ziarani China
2 Februari 2012Kansela Angela Merkel wa Ujerumani,akiwa ziarani mjini Beijing amewasihi viongozi wa jamhuri ya umma wa China watumie ushawishi wao kuitanabahisha Iran iachilie mbali mpango wake wa kinuklea unaozusha mabishano.
Kansela Merkel aliyekuja kusaka uungaji mkono wa Beijing katika kupambana na mgogoro wa madeni katika zoni ya Euro,alikuwa na mazungumzo ya muda mrefu pamoja na rais Hu Jintao na waziri mkuu Wen Jiabao kuhusu vikwazo dhidi ya Iran.
Akizungumza na waandishi habari mwishoni mwa hotuba yake mbele ya chuo cha sayansi jamii mjini Beijing,kansela Angela Merkel amesema:atapigania fikra kama ulaya kwa mfano inaweka vikwazo,China nayo itumie ushawishi wake ili kuiambia Iran:"hatuhitaji na wala tusiruhusu kuwepo dola jengine la kinuklea."
China,nchi inayoagizia mafuta mengi zaidi ya Iran,inapinga vikwazo dhidi ya Iran kinyume na Umoja wa Ulaya ulioamua wiki iliyopita kusitisha kuagizia mafuta kutoka Iran.
Mnamo siku ya kwanza ya ziara yake hii ya siku tatu,kansela Angela Merkel amezungumzia pia mgogoro wa madeni unaoikaba zoni ya Euro tangu miaka miwili iliyopita,akisistiza,hili si tatizo linaloihusu Ulaya peke yake,bali tatizo la ulimwengu mzima ambalo jamhuri ya umma wa China inaweza kuchangia kulipatia ufumbuzi.
"Sarafu ya Euro imeifanya Ulaya kuwa na nguvu" amesema kansela Angela Merkel katika hotuba yake mbele ya chuo cha Sayansi jamii mjini Beijing akizungumzia "miradi mikubwa mikubwa iliyotekelezwa na Umoja wa ulaya katika kipindi cha miaka miwili iliyopita.
"Mashindano ya kimataifa yamekuwa magumu miaka ya hivi karibuni na Ulaya inabidi ijiambatanishe" amesisitiza kansela Angela Merkel na kuongeza "ana hakika mageuzi yaliyoanzishwa na Umoja wa ulaya ni ya maana."
Kansela Angela Merkel amezungumzia pia kuhusu haki za binaadam akisema Ujerumani na China zinaendeleza mdahalo wa maana na kubadilishana maoni kuhusu masuala tofauti.
Kuhusu Syria kansela Merkel amesema wakati umewadia kwa jumuia ya kimataifa kuweka kando tofauti zao na kufikia msimamo wa pamoja katika umoja wa mataifa.
Kansela Angela Merkel na ujumbe mkubwa wa wafanyabiashara,amepangiwa kwenda Kanton kesho,mji mkuu wa kiuchumi,kusini mwa jamahuri bya umma wa china.
Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/Afp/Reuters/dapd
Mhariri:Yusuf Saumu