1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Kansela Merkel asema Georgia itajiunga na NATO ikiwa tayari

Saumu Mwasimba17 Agosti 2008

Aitaka Urussi kuondoa mara moja wanajeshi wake Ossetia Kusini

https://p.dw.com/p/Ez0d
Merkel amuhakikishia rais Saakashvli uungaji mkonoPicha: AP

Kansela Angela Merkel wa Ujerumani amesema kwamba Georgia itajiunga na jumuiya ya kujihami ya nchi za magharibi NATO.Tamko la Merkel ndio la kwanza ambalo ni zito katika uungaji mkono wa Georgia tangu kuibuka kwa mzozo kati ya nchi hiyo na na Urusi.Aidha Kansela Merkel ameitaka Urussi iondoe majeshi yake mara moja na kuzingatia makubaliano ya kusitisha mapigano yaliyofikiwa chini ya usimamizi wa Ufaransa.Merkel amesema''Tunatambua hadhi ya utaifa ya Georgia pamoja na maeneo yake na inabidi hilo liheshimiwe kama inavyofanyika kwa nchi nyingine yoyote.tunaunga mkono mpango wa amani uliofikiwa na tunataraji makubaliano hayo yatatekelezwa''

Merkel pia amethibitisha kwamba mazungumzo yanaendelea juu ya kuweka wanajeshi wa kulinda amani wa umoja wa ulaya katika jimbo la Ossetia.Wakati hayo yakiarifiwa rais wa Urusi Dmitry Medvedev ametangaza kwamba wanajeshi wake wataanza kuondoka Ossetia Kusini jumatatu.

Awali kulikuweko na taarifa za kutatanisha juu ya kuondoka kwa wanajeshi hao wa Urusi,kamanda wa urussi wa kikosi kinachohusika kwenye mzozo huo Generali Vyachislav Borisov awali alifahamisha kwamba wanajeshi wake wameanza kuondoka kutoka mji mkuu wa Ossetia Kusini wa Tskinvali.

Baadae wizara ya ulinzi ya Urussi ikakanusha ripoti hiyo ikisema hatua hiyo itatokana na hali ya usalama katika eneo hilo.

Awali rais George W Bush wa Marekani aliikaribisha hatua ya Urussi ya kufikia makubaliano ya kusimamisha vita yaliyosimamiwa na Ufaransa lakini akasema huenda kusiweko mjadala wowote juu ya hadhi ya utaifa wa Gergia kuhusiana na majimbo yake yaliyojitenga.

Wakati huohuo Georgia imefahamisha kuwa waasi wa jimbo la Abkhazia na wanajeshi wa Urussi bado wanadhibiti vijiji kadhaa vya Georgia.