Hali nchini Misri-wanajeshi waomba radhi
24 Novemba 2011Katika wakati ambapo machafuko yalipamba moto jana usiku katika uwanja wa Tahrir,kituo cha televisheni cha Al Jazira,kilisema waziri wa mambo ya ndani Mansour al Essaoui alishauri duru ya kwanza ya uchaguzi iliyopangwa kuanza jumatatu ijayo,iakhirishwe.Ripoti hiyo lakini haikuthibitishwa hadi sasa,seuze tene mkuu wa baraza la kijeshi Marshal Mohammed Hussein Tantawi alihakikisha katika hotuba yake kwa taifa jumanne iliyopita,uchaguzi huo utafanyika kama ilivyopangwa.
Watu 39 wanasemekana wameuwawa tangu wimbi hili jipya la machafuko lilipoanza kupiga jumamosi iliyopita.
Jana usiku risasi zilifyetuliwa karibu na wizara ya mambo ya ndani-kitovu cha utawala wa kijeshi ambao ndio chanzo cha kilio cha waandamanaji waliokusanyika Tahrir.Mashahidi wanasema kuna watu waliouwawa.
"tulikuwa tunasali,wakaanza kutufyetulia gesi za kutoa machozi.Tulipokimbia wakatufyetulia risasi hasa."
Viongozi wanakanusha kwamba risasi zimetumiwa dhidi ya waandamanaji.Waziri wa mambo ya ndani amesema kupitia televisheni ya taifa watu wasiojulikana walifyetua risasi wakiwa juuu ya mapaa ya nyumba zinazouzunguka uwanja wa Tahrir.
Waandamanaji wanawatuhumu viongozi wa kijeshi kuwaajiri wafanya fujo kwa lengo la kuwafedhehesha.
Ridhaa zilizotolewa jumanne usiku na Marshal Tantawi na baraza kuu la kijeshi,kuitisha uchaguzi wa rais miezi sita kabla,,kuunda serikali mpya ya mpito na ahadi uchaguzi utakuwa huru,hazikusaidia kutuliza kilio cha waandamanaji katika uwanja wa Tahrir.
Baraza kuu la kijeshi limeomba radhi hii leo kupitia mtandao wake wa Facebook kwa hasara ya maisha iliyopatikana wakati wa machafuko kati ya wanaharakati wanaodai mageuzi na vikosi vya usalama.
Na mkuu wa shirika la haki za binaadam la Umoja wa Mataifa Navi Pillay ametoa mwito uchunguzi huru ufanywe kuhusu machafuko ya hivi karibunui nchini Misri,.
Mwandishi:Hamidou Oummilkheir/Reuters/Afp
Mhariri: Abdul-Rahman,Mohammed