1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Guterres aionya Israel dhidi ya kuivamia Rafah

Tatu Karema
16 Februari 2024

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, António Guterres, ameionya Israeli kuhusu athari za kufanya mashambulizi ya ardhini kwenye mji wa kusini mwa Gaza, Rafah, ambako Wapalestina milioni 1.3 walikimbilia kutafuta hifadhi.

https://p.dw.com/p/4cUTn
Ujerumani | Mkutano wa Usalama wa Munich 2024 | Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa  Antonio Guterres
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, akizungumza kwenye Mkutano wa Usalama wa Munich siku ya Ijumaa (16 Februari 2024).Picha: Johannes Simon/Getty Images

Akizungumza kwenyeMkutano Kimataifa wa Usalama mjini Munich nchini Ujerumani siku ya Ijumaa (Februari 16), Guterres alisema kuwa mji wa Rafah uko katika kitovu cha operesheni za msaada wa kiutu za Umoja wa Mataifa na kwamba operesheni kubwa ya kijeshi ya Israel mjini humo itakuwa na athari kubwa.

Soma zaidi: Guterres kufunguwa Mkutano wa Usalama wa Munich

"Operesheni ya misaada ya kibinadamu sasa inakabiliwa na hali ngumu zaidi na wafanyakazi wa msaada wanafanya kazi kwenye mazingira duni ikiwa ni pamoja na vizuizi katika eneo hilo, vikwazo vya Israel, na hali ya kutokuwepo kwa usalama." Alisema Katibu Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa.

Guterres amerejea pia wito wake wa kuachiliwa mara moja na bila masharti kwa mateka wote na kukomesha mapigano ili msaada wa kibinaadamu upelekewe eneo hilo, akisema hiyo ndiyo "njia pekee ya kuongeza kwa kiasi kikubwa utoaji wa misaada huko Gaza."