1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

COP15: Bado hakujafikiwa mafanikio makubwa

13 Desemba 2022

Mkutano wa COP15 kuhusu bioanuwai unaoendelea mjini Montreal nchini Canada haujafikia mkataba wa kihistoria wa kukomesha uharibifu wa mazingira, na ikiwa zimesalia siku nne, hadi sasa hakuna mafanikio makubwa.

https://p.dw.com/p/4KrTh
UN-Artenschutzkonferenz COP 15 in Montreal, Kanada 2022 | Themenbild
Picha: Christina Muschi/REUTERS

Maoni ya wengi yanabaini kuwa mazungumzo hayo yatakuwa magumu zaidi siku ya Alhamisi, wakati mawaziri wa mazingira kutoka kwa wanachama 196 wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa bioanuawi (CBD), watakapochukua nafasi kutoka kwa wajumbe wao huko Montreal.

UN-Artenschutzkonferenz COP 15 in Montreal, Kanada 2022 | Antonio Guterres, UN-Generalsekretär
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres akihuubia mkutano wa COP15 nchini Canada.Picha: Andrej Ivanov/AFP/Getty Images

Lakini uwezekano wa kufikia makubaliano mnamo Desemba 19 kuhusu "mkataba wa kuheshimisha mazingira", unaojumuisha malengo 20 ya kukomesha uharibifu wa maji, misitu na viumbe hai ifikapo mwishoni mwa muongo huu, utakuwa hafifu ikiwa rasimu ya makubaliano hayo itasalia kama ilivyo sasa.

Soma zaidi: COP15: Bioanuwai ni nini na kwa nini ni muhimu sana?

Licha ya wajumbe 5,000 kujadiliana kwa muda mrefu tangu Desemba 3, rasimu hiyo bado haijakamilika huku mada kadhaa zikiwa bado mezani. Hadi sasa, malengo matano pekee  kati ya 22 au 23 yaliyotarajiwa ndiyo yaliyopatiwa ufumbuzi.

Alfred DeGemmis, afisa mkuu katika Jumuiya ya Kuhifadhi Wanyamapori (WCS) amesema kuwa wajumbe wa Serikali wanapiga hatua, lakini si kwa kasi ya kutosha ili kufikia kuandaa rasimu kamili kabla ya kuwasili kwa mawaziri.       

Soma zaidi:COP15: Kampuni zatakiwa kutangaza madhara yao kwa mazingira 

UN-Artenschutzkonferenz COP 15 in Montreal, Kanada 2022 | Justin Trudeau, Kanada
Waziri Mkuu wa Canada, Justin Trudeau akihutubia mkutano huo wa bioanuawi huko Montreal, Canada.Picha: Christina Muschi/REUTERS

Muda unatutupa mkono: aina ya wanyama milioni moja iko hatarini kutoweka, theluthi moja ya ardhi imeharibiwa vibaya, rutuba ya udongo na maji safi viko hatarini, huku bahari zikitishiwa na uchafuzi wa mazingira na mabadiliko ya hali ya hewa.

Marco Lambertini, mkuu wa shirika la kimataifa la kulinda wanyamapori WWF, amesema bado wako mbali kufikia rasimu hiyo, lakini wanakaribia kuikamilisha. Ameongeza kuwa, tangu kuanza kwa mazungumzo hayo, ameshuhudia juhudi endelevu.      

Tatizo la ufadhili kwa mataifa yanayoendelea

Kwa upande wake Sebastien Treyer, mkurugenzi mkuu wa taasisi ya utafiti ya IDDRI amesema kumekuwa kukiibuka msukumo wa nchi za Kusini mwa dunia, kutaja kuwa hazitakubali kudiriki katika makubaliano yoyote bila ya kupewa ufadhili unaostahiki.   

Soma zaidi:  Mkutano wa Bayoanuwai COP15 wafunguliwa Canada   

Siku ya Jumamosi, Brazil ilisisitiza, kwa niaba ya bara la Afrika na nchi nyingine 14 zikiwemo India na Indonesia, maombi yao ya "ruzuku ya kifedha ya angalau dola bilioni 100 kwa mwaka au asilimia moja ya Pato la dunia hadi ifikapo mwaka 2030."

Elfenbeinküste | COP15 in Abidjan
Alain-Richard Donwahi, Waziri wa zamani wa maji na misitu wa Ivory Coast ambaye pia ndie Mwenyekiti wa Mkutano wa COP15 huko Canada.Picha: Sia Kambou/AFP/Getty Images

Nchi tajiri zimekuwa zikionyesha kuwa ongezeko hilo halitowezekana wakati misaada yake iliyotengwa kwa ajili ya bioanuwai mnamo mwaka 2020 ilifikia tu dola bilioni 10.

Soma zaidi: Wanaharakati wataka miito yao kulinda bayoanuwai isikizwe

Mjumbe wa Ufaransa kwenye mkutano huo wa COP15, Sylvie Lemmet, ameonya kuwa, kuzungumzia ghafla tu kuhusu kitita cha bilioni 100 kunayafifisha malengo ya mazungumzo hayo hasa ikizingatiwa kuwa kwa sasa msaada uliyofikiwa ni bilioni 10 huku nchi tajiri zikiwa pia zimeahidi kuongeza misaada ya maendeleo katika muongo mmoja uliopita.

Umoja wa Ulaya pia unapinga kuundwa kwa hazina mpya ya kimataifa ya bioanuwai, jambo ambalo litakuwa kipaumbele kwa nchi kadhaa kwenye mkutano mwengine wa COP16 utakaofanyika mwaka 2024 nchini Uturuki.