1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

China kuendelea kufuata nadharia ya Karl Marx

Zainab Aziz
4 Mei 2018

China daima itakuwa mlinzi na mtekelezaji wa falsafa yake. Hayo ameyatamka rais wa China Xi Jinping alipotoa hotuba rasmi bungeni ya kumuenzi Karl Marx katika mandalizi ya kuadhimisha miaka 200 tangu kuzaliwa kwake.

https://p.dw.com/p/2xBoA
China Rede Xi Jinping zum 200. Geburtstag von Karl Marx
Picha: Reuters/J. Lee
Rais wa China Xi Jinping
Rais wa China Xi JinpingPicha: Reuters/J. Lee

Katika hotuba yake, Rais Xi Jinping aliwataka wanachama wa chama cha kikomunisti wapalilie tabia ya kusoma nadharia za Marx na Karl Marx wazingatie tabia hiyo kuwa utaratibu wa maisha yao na melengo ya moyoni.  Nadharia za Karl Marx bado zinaendelea kuwa na uzito nchini China licha ya miongo kadhaa ya sera za uchumi wa soko zinazotekelezwa nchini humo. Na kutokana na sera hizo China ni nchi ya pili duniani yenye nguvu za  kiuchumi. Wanafunzi wanaanza kujifunza nadharia za mwanafalsafa huyo wa Ujerumani kwenye shule za upili. Watumishi wa serikali na hata waandishi wa habari wanalazimika kuchukua masomo juu ya Karl Marx ili kuweza kupanda madaraja kazini.

Hata hivyo, urithi wa mwanamapinduzi huyo wa Kijerumani unaendelea kuwagawa watu duniani na pia katika nchi yake ya uzawa. Lakini gazeti la serikali  la Peoples' Daily limesema, nchini China kumbukumbu ya mwaka wa 200 tangu kuzaliwa kwa Marx ni fursa ya kuutathmini moyo wa nadharia miongoni mwa watu wa nchi hiyo.

Mandalizi ya miaka 200 tangu kuzaliwa Karl Marx katika mji wake wa uzawa wa Trier
Mandalizi ya miaka 200 tangu kuzaliwa Karl Marx katika mji wake wa uzawa wa TrierPicha: picture-allilance/dpa/H. Tittel

Pamoja na shughuli zitakazofanyika hapo kesho kwa ajili ya maadhimisho ya Marx ni kutangazwa katika vyombo vya serikali, mfululizo wa filamu za matukio zinazoitwa nasaha za Marx ni sahihi. China pia ilitoa zawadi ya sanamu ya shaba ya Karl Marx kwa mji wa uzawa wa mwanamapinduzi huyo wa Trier ulioko magharibi mwa Ujerumani ambako kazi zake zinaendelea kuwa za mikingamo, na hasa miaka 25 baada ya kuanguka kwa ukuta wa Berlin.

China ndiyo nchi kubwa kabisa duniani inayojitambulisha kuwa ya Kisoshalisti, tangu kusambaratika kwa Umoja wa Kisoviet na kampuni zinazomilikiwa, na serikali zinaendelea kuhodhi sekta kuu za uchumi. Hata hivyo, China inao mabilionea 370 ikiwa ni nchi ya pili baada ya Marekani. Wakati huo huo, tofauti za hali ya maisha kati ya watu wa mijini na mashambani zimeendelea kuwa kubwa  katika miaka ya hivi karibuni.

Maandalizi ya miaka 200 tangu kuzaliwa Karl Marx
Maandalizi ya miaka 200 tangu kuzaliwa Karl MarxPicha: picture-allilance/dpa/H. Schmidt

Mitindo ya kibepari ikiwa ni pamoja na bidhaa za anasa ziliofurika nchini humo, tangu kufanyika kwa mageuzi mwishoni mwa miaka ya 70 imewafanya wachambuzi wahoji kwamba chama cha Kikomunisti kinatoa kauli tu juu ya Usoshaliti na kwamba mahitaji ya kiuchumi yamefunika itikadi.  Lakini rais wa China, Xi Jinping, amekanusha madai ya wakosoaji hao na kusema kuwa chama cha  Kikomunisti kiko sahihi kabisa katika kulibeba bango la Karl Marx.

Wasomi wa China wanasema ni kutokana na falsafa ya Marx kwamba nchi yao imeweza kuwaondoa watu zaidi ya milioni 500 kutoka kwenye umasikini. Profesa wa isimu za lugha na utamaduni Zhang Yuwu amesema nadharia za Karl Marx zimeiwezesha China kupata njia mahsusi ya kuleta usasa kwa watu wake.

Mwandishi: Zainab Aziz/AFPE

Mhariri: Mohammed Khelef