BRUSSELS: Umoja wa Ulaya hautadhamini usafirishaji wa mafuta kwenda Gaza
20 Agosti 2007Matangazo
Umoja wa Ulaya hautadhamini usafirishaji wa nishati katika Ukanda wa Gaza ikiwa kundi la Hamas litaanza kutoza kodi kwa nishati ya umeme katika eneo hilo.
Msemaji wa umoja huo, Antonia Mochan amesema leo mjini Brussels, Ubelgiji kwamba uamuzi wa kusitisha malipo Alhamisi iliyopita kwa ajili ya usafirishaji wa mafuta kwenda katika kituo kikubwa cha umeme cha Ukanda wa Gaza, ulichukuliwa kwa sababu za usalama, hususan kuhusiana na hali ya wasiwasi katika vivuko vya mpakani.
Uamuzi huo umechukuliwa huku kukiwa na wasiwasi kwamba kundi la Hamas huenda likatoza kodi umeme ili liipatie fedha serikali yake.