BREMEN: Mawaziri wa mambo ya kigeni wa Umoja wa Ulaya wakutana
30 Machi 2007Matangazo
Mawaziri wa mashauri ya kigeni wa nchi za Umoja wa Ulaya wanakutana leo mjini Bremen kaskazini mwa Ujerumani kujadili mpango wa amani wa Mashariki ya Kati.
Viongozi hao watajaribu kufikia msimamo mmoja juu ya serikali mpya ya umoja wa kitaifa ya mamlaka ya Palestina.
Mazungumzo hayo ambayo sio rasmi, yanaoongozwa na waziri wa mashauri ya kigeni wa Ujerumani, Frank Walter Steinmeier, na yataamua ikiwa Umoja wa Ulaya utakuwa na mawasiliano na serikali mpya ya Wapalestina.
Mawaziri hao pia wanataka kujadili hatima ya jimbo la Kosovo kabla mkutano wa baraza la usalama la Umoja wa Mataifa utakaojadili swala hilo.
Jana bunge la Ulaya liliunga mkono mpango unaodhaminiwa na Umoja wa Mataifa unaotaka kulipa uhuru jimbo la Kosovo kutoka kwa Serbia.