BERLIN: Merkel ataka Ujerumani iongeze juhudi kuboresha uchumi
1 Januari 2007Matangazo
Kansela wa Ujerumani Bi Angela Merkel amesema Ujerumani inatakiwa kuongeza marudufu juhudi zake katika mwaka huu mpya wa 2007 ikiwa inataka kuendelea kuufua uchumi wake.
Katika ujumbe wake wa mwaka mpya, Bi Merkel amesema serikali yake itaendeleza mijadala ya mageuzi katika jamii na soko ajira. Aidha amesema ufanisi hautapatikana bila kupitia mitihani migumu.
Kuhusu sera za kigeni kansela Merkel amesema Ujerumani italenga kuyafufua mazungumzo ya amani ya mashariki ya kati na katiba ya Umoja wa Ulaya wakati Ujerumani itakapokuwa rais wa umoja huo na rais wa mataifa ya G8.
Ameonya kwamba Ulaya iliyoungana pamoja itafaulu kukabiliana na changamoto za utandawazi, ugaidi na vita.