1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ziara ya Ahmadinedjad nchini Irak na vikwazo vya baraza la usalama dhidi ya nchi yake

Philipp, Peter DW4 Machi 2008

Marekani na Iran wanaendelea kupimana nguvu

https://p.dw.com/p/DHua
Rais Ahmadinedjad wa iran na waziri mkuu Nur el Maliki wa IrakPicha: AP


Rais Ahmadinedjad wa Iran ameitembelea kwa mara ya kwanza Irak na kufikia makubaliano ya ushirikiano wa dhati kati ya nchi hizo mbili.Marekani imeipuuza ziara hiyo na badala yake imelishawishi kwa mara ya tatu baraza la usalama la umoja wa mataifa lizidishe makali ya vikwazo vya Umoja wa mataifa dhidi ya jamhuri hiyo ya kiislam.


Azimio jipya la baraza la usalama la umoja wa mataifa na ziara iliyomalizika hivi punde, ya kwanza kuwahi kufanywa na rais Mahmoud Ahmadinedjad wa Iran nchini Irak,kimsingi si mambo yanayofungamana,-lakini kindani ndani mtu anaweza kusema hasha,yanafungamana.Hakuna chochote chengine kinachoweza kumulika vyema zaidi hali ya mambo,kuliko matukio haya mawili.Katika malumbano yao yasiyokwisha,wa-Iran na wa-Marekani,kila mmoja amejikingia pointi-maendeleo ya kweli lakini hayakupatikana,si kwa upande mmoja na wala si kwa upande wa pili.


Hivyo basi rais wa Iran kwa kufanya ziara ya kihistoria mjini Baghdad-eneo ambalo kimsingi liko chini ya ulinzi wa Marekani,amethibitisha kwamba yeye na Iran wana jukumu kubwa katika eneo hilo na kwamba Washington ingefanya kosa kubwa,pindi ingepuuza ukweli huo.

Na Washington pia imefanikiwa kulitanabahisha baraza la usalama la Umoja wa mataifa-tukiitenga nchi moja ambayo haikupiga kura upande wowote- lizidishe makali ya vikwazo vilivyopitishwa tangu zamani dhidi ya Iran- na kudhihirisha wakati huo huo kwamba katika mvutano wa mradi wa kinuklea wa Iran,wa Marekani wanaendelea kuvuta kamba na wala hawatachoka   licha ya ukakamavu wa wairan.


Rais Bush ameridhishwa kuona kwamba hata Urusi na jamhuri ya umma wa China safari hii wameunga mkono azimio hilo la baraza la usalama bila ya kutoa masharti.Zilikua nchi hizo hizo ambazo siku za nyuma zilisimama kidete  kwa masilahi yao wenyewe ya kiuchumi kupinga aina yoyote ya vikwazo dhidi ya Teheran.


Lakini  inamaanisha nini kusimama kudete kwaajili ya Iran?Tangu mapema mwaka huu ilijulikana wazi kabisa kwamba vikwazo vipya vitawekwa dhidi ya Iran,baada ya wanachama watano wa kudumu wa baraza la usalama pamoja na Ujerumani kufikia makubaliano mjini Berlin.Lakini vikwazo hivyo si pigo kwa Iran.Baadhi ya viongozi na makampuni ya Iran wamejumuishwa katika orodha nyeusi na bidhaa ya bidhaa kuzuwiliwa zisiingie Iran lakini hakuna mtu yoyote mjini New York na Washington anaeamini kwa dhati kwamba Teheran itatishika na kubadilisha msimamo wake.Wametaka kuonyesha tuu jinsi wanavyokerwa na msimamo wa Iran-hakuna la ziada.


Viongozi wa Iran hawatotaharuki.Bila ya kujali lengo la mpango wa kinuklea wa Iran ni nini:wairan wanaendelea kuamini mpango huo ni wa amani uliolengwa matumizi ya kiraia na kwamba ni haki yao kabisa kurutubisha maadini ya uranium.


Ni hoja inayoingia akilini.Ikiwa mojawapo ya nchi iliyotia saini makubaliano ya kutosambaza silaha za kinuklea,Iran ina haki pia ya kurutubisha maadini hayo kwa sharti hayendi kinyume na makubaliano hayo na kwa namna hiyo haistahiki pia kuwekewa vikwazo.


Ingawa imetajwa kwamba Iran inakwenda kinyume na makubaliano hayo,lakini ushahidi mpaka sasa haujapatikana.Kwa namna hiyo viongozi wa mjini Teheran wanapata nguvu wanapodai ni chuki za Marekani tuu dhidi yao.Na hoja hizo zinasikilizwa hata nje ya mipaka ya Iran,tangu katika ulimwengu wa kiarabu mpaka katika nchi jirani hasimu mkubwa wa zamani Irak.