1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Yajue majumu ya rais wa Ujerumani

Sudi Mnette
12 Februari 2017

Tangu Donald Trump alipokabidhiwa hatamu za uongozi nchini Marekani, wengi wanajiuliza madaraka ya aina gani anadhibiti rais wa Marekani. Hali ni tofauti nchini Ujerumani: Kutokana na historia wadhifa huo ni uwakala.

https://p.dw.com/p/2XQp9
Berlin Wahl des Bundespräsidenten  Frank-Walter Steinmeier
Picha: picture alliance/AP Photo/Markus Schreiber

Rais wa shirikisho ndie kiongozi wa taifa lakini sio kiongozi mwenye madaraka makubwa katika muundo wa uongozi nchini Ujerumani. Wadhifa na jukumu ni mambo yaliyopunguzwa nguvu kutokana na yaliyotokea wakati wa utawala wa wanazi nchini Ujerumani. Viongozi wametaka kuondowa uwezekano wa kumuona mwakilishi wa ngazi ya juu wa Ujerumani akijikuta na madaraka yote mikononi mwake.Hali hiyo inatofautisha madaraka ya rais wa shirikisho na yale waliyokuwa nayo marais wa enzi za Reich katika jamhuri ya Weimar kati ya mwaka 1918 hadi 1933.

Rais wa shirikisho wa enzi hizi mpya hatawali,anaiwakilisha nchi. Anapofanya ziara rasmi nchi za nje,rais wa shirikisho anageuka kuwa "wajihi na sauti ya Ujerumani." Nchini anawakilisha umoja wa taifa,kama ilivyothibitishwa na korti ya katiba mnamo mwaka 2014.Na ili kuweza kudhamini umoja wa taifa,rais wa shirikisho mara zote hujiweka kando ya mizozo ya kisiasa ya vyama. Shughuli zake hazielemei upande wa chama chochote.Katika hotuba zake anatilia mkazo yaliyotajwa katika katiba ya Ujerumani na sheria msingi. Rais wa shirikisho hulazimika kujitoa katika chama cha kisiasa kwa muda wote anaoendesha majukumu yake.

Madaraka ya rais wa shirikisho

Deutschland | Wahl des Bundespräsidenten | Frank-Walter Steinmeier
Rais mpya wa shirikisho la Ujerumani, Frank-Walter SteinmeierPicha: picture-alliance/dpa/G. Fischer

Madaraka ya rais wa shirikisho ni kiunganisho kati ya nguzo tatu za upongozi,serikali,bunge na mahakama. Kwa namna hiyo rais wa shirikisho anaweza kutoa msukumo katika masuala kuhusiana na demokrasia na pia taifa linaloheshimu sheria. Hali hii amejionea pia rais aliyemaliza mhula wake Joachim Gauck. Amekiri kwamba wadhifa wa rais wa shirikisho umemfanya ajiamini zaidi, azidishe maarifa yake na kutambua kwamba majukumu yote ya kisiasa hayako mabegani mwake. "Mtu anakuwa huru kutamka wazi kabila hili au lile" amesema Joachim Gauck.

Rais wa shirikisho anapotoa hutuba zake na nasaha ni kwaajili ya kusaidia kusaka ufumbuzi wa mizozo ya ndani na pia ya kimataifa. Anatoa msukumo lakini siasa hali ya nje inasalia kuwa jukumu la serikali kuu na mawaziri wake. Mara nyingi rais wa shirikisho hutoa shinikizo katika kuheshimiwa haki za binaadam, kuhimiza dola linaloheshimu sheria na kuendelezwa midahalo kwa njia za kidemokrasi..Pia katika juhudi za kuimarisha amani,kupambana na ugaidi,kuimarisha umoja wa Ulaya na ulinzi wa mazingira na mabadiliko ya tabia nchi ni miongoni mwa majukumu ya rais wa shirikisho.

Shirikisho la jamhuri ya Ujerumani linapotia saini makubaliano, basi na rais wa shirikisho pia anabidi atie saini yake kwa niaba ya wananchi. Hali hiyo inahusu pia sheria,zinazopitishwa na bunge la shirikisho Bundestag na baraza la wawakilishi wa majimbo Bunderat.Rais wa shirikisho anapoweka saini yake tu ndipo sheria hizo zinapoweza kuanza kufanya kazi.Rais wa shirikisho anaangaliwa pia kuwa wakili wa demokrasia na anabidi atoe kauli ya m wisho kama sheria iliyopitishwa inafungamana pia na mwogozo wa sheria msingi.

Panapotokea mizozo rais wa shirikisho anakuwa na jukumu maalum.Kwa mfano yeye ndie anaeitisha uchaguzi mpya ikiwa kansela atakosa uungaji mkono wa bunge. Rais wa shjirikisho ndie anaependekeza bungeni nani achaguliwe kuwa kansela,mawaziri sawa na mawakilishi na maafisa wa ngazi ya juu serikalini na jeshini. Rais wa shirikisho ni mdhamini pia wa maonyesho kadhaa. Anawaalika mabalozi wa nchi za nje na kupokea hati zao za kuchaguliwa kama mabalozi.

Mwandishi: Fuchs Richard/Hamidou Oumilkheir
Mhariri:Josephat Charo