Waziri wa Ulinzi wa Ujerumani akosolewa na upinzani
15 Desemba 2009amejitetea kwa kusema kuwa upanzani pia ulikuwa na habari zile zile alizoarifiwa.
Habari zinazochomoza hadharani kuhusika na shambulizi la anga la Kundus zinazidi kutatanisha. Habari mpya zinaeleza dhamira ya shambulio la Septemba 4, lililoamriwa na kanali Georg Klein wa jeshi la Ujerumani. Shambulio hilo halikulenga tu malori mawili ya jeshi la Ujerumani "Bundeswehr" bali hata Wataliban waliozunguka malori hayo ya mafuta - "wauawe" Hivyo ndio vyombo vya habari vya Ujerumani vilivyonukulu amri ya kanali Klein kuambatana na ripoti ya NATO. Upande wa upinzani umehamakishwa na habari hizo mpya, zilizothibitishwa na Waziri wa Ulinzi Karl-Theodor zu Guttenberg.
Kiongozi wa chama cha Kijani Claudia Roth amesema sera za serikali kuu kuhusu utoaji wa habari ni "aibu" na kuongezea:
"Bunge na wananchi - wote wanadanganywa na serikali. Tunahitaji uwazi kwani hili si suala la hivi hivi tu - ni suala la maisha na kifo na hapo kunahitajiwa imani na uaminifu."
Vyama vyote upinzani vinamtuhumu waziri wa ulinzi kuwa ameudanganya umma. Lakini Waziri Karl-Theodor zu Guttenberg amekanusha tuhuma hizo na amesema:
"Hata upande wa upinzani angalau kuanzia Novemba 3,ulikuwa na fursa ya kuiona ripoti ya NATO. Ripoti hiyo ilipokewa na upande wa upinzani."
Kwa hivyo amesema,upinzani pia ungeweza kufahamu kuwa Wataliban nao walilengwa katika shambulio hilo la anga.Lakini kiongozi wa chama cha SPD, Sigmar Gabriel anaetoa mwito wa kumtaka Guttenberg ajiuzulu amesema kuwa si wajibu wa upinzani kuuarifu umma kuhusu shambulio lililouwa hadi watu 140. Kwa maoni ya Gabriel, habari mpya zilizoibuka zinazusha suala iwapo mkakati wa jeshi la Ujerumani nchini Afghanistan umebadilishwa ili viongozi wa Taliban waweze kulengwa na kuuawa hata ikiwa si kitisho kwa wanajeshi wa Ujerumani au kazi zao. Ikiwa hiyo ni kweli basi anataka kujua nani alietoa amri na nani aliejua kuhusu badiliko hilo.
Sasa nchini Ujerumani, wanasiasa na wanasheria wanauliza iwapo hatua hiyo inakiuka mamlaka ya bunge na haki ya binadamu. Lakini msemaji wa serikali Ulrich Wilhelm anasema fikra kuwa kimsingi jukumu la jeshi la Ujerumani nchini Afghanistan limebadilishwa si sahihi. Masuala yote mengine amesema, yatashughulikiwa na kamati ya uchunguzi itakayoanza kufanya kazi yake siku ya Jumatano. Hiyo haiwaridhishi wananchi kwani kamati hiyo itakutana kwa siri.
Mwandishi:Werkhäuser.N/ZPR/P.Martin
Mhariri/Mtullya Abdu