1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Watoto wanaozaliwa nchi maskini wakabiliwa na hatari ya kifo

Sylvia Mwehozi
20 Februari 2018

Ripoti ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuwahudumia watoto UNICEF, inaonyesha kuwa watoto wanaozaliwa katika nchi maskini zaidi duniani wengi kutoka Afrika wanakabiliwa na hatari ya kifo ikilinganisha na wa nchi tajiri.

https://p.dw.com/p/2sxxj
Somalia Krise - Hungersnot und Cholera
Picha: picture-alliance/AA/A. Hudaverdi

Mkurugenzi mtendaji wa UNICEF Henrietta Fore amesema wakati robo ya mwisho ya karne imeshuhudia maboresho makubwa katika afya ya watoto wakubwa, jitihada zimekuwa ndogo kutokomeza vifo vya watoto chini ya mwezi mmoja, akiongeza kwamba vifo vingi vinazuilika.

Kati ya nchi 10 ambazo ziko katika hatari kubwa, 8 ni kutoka kusini mwa Afrika mwa jangwa la sahara ambako mama mjamzito ana uwezekano mdogo wa kupata msaada kwa sababu ya umaskini, migogoro au taasisi dhaifu kwa mujibu wa ripoti hiyo.

Nchi hizo 8 ni pamoja na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Somalia, Lesotho, Guinea-Bissau, na Sudan Kusini. Nyingine ni Cote d'Ivoire, Mali na Chad. Kila mwaka watoto karibu milioni 2.6 hawanusuriki katika mwezi wao wa kwanza baada ya kuzaliwa.

Ripoti hiyo imezinduliwa sanjari na uzinduzi wa kampeni ya kidunia iliyopewa jina la "kila mtoto hai" inayolenga kuhakikisha upatikanaji wa suluhusho la huduma bora za afya kwa kila mama na mtoto". Zaidi ya asilimia 80 ya vifo vya watoto wachanga vinazuilka, inasema ripoti hiyo, "kwa upatikanaji wa wakunga waliopatiwa mafunzo, pamoja na ufumbuzi mwingine kama upatikanaji wa maji safi, kemikali za kuua viini vya maradhi, unyonyeshaji wa maziwa ya mama ndani ya saa moja ya kwanza, na mlo mwema".

Zentralafrikanische Republik Mutter mit Baby
Mama na mtoto Jamhuri ya Afrika ya KatiPicha: Getty Images/AFP/R. Kaze

Lakini uhaba wa wakunga na wafanyakazi wa afya wenye mafunzo bora ni tatizo kubwa katika mataifa yaliyo maskini. Wakati nchi tajiri kama Norway ina madkatari 18, wauguzi na wakunga kwa kila watu 10,000, nchi maskini kama Somalia ina mtaalamu mmoja.

Tangu maboresho ya afya yanaweza kuwa ghali" ni muhimu sana kuwekeza fedha kwa njia nzuri", amesema Willibald Zeck, mshauri mwandamizi wa UNICEF .

Rwanda nchi ya Afrika yenye huduma bora y afya kwa watoto

Hata hivyo, kati ya nchi ambazo zimefanya maboresho makubwa ni Rwanda, ambayo zaidi ya nusu ya kiwango chake kimepungua kuanzia 1990 hadi 2016, ikionyesha kwamba "utashi wa kisiasa wa kuwekeza katika mifumo ya afya yenye nguvu ni muhimu," imesema ripoti hiyo .

Masuala ya elimu, pia yanahusika. Watoto waliozaliwa na mama wasio na elimu huwa karibu mara mbili  katika hatari ya kufa mapema ikilinganishwa na watoto wachanga waliozaliwa na mama wenye elimu ya sekondari. Marekani kwa ujumla ambayo ina utofauti wa mapato na tofauti kubwa katika upatikanaji wa huduma za afya ilikuwa ni nchi ya 41 iliyo salama zaidi kwa watoto wachanga.

Nchi zenye viwango vya chini katika vifo vya watoto wachanga baada ya Japan, ziadi ni zile zilizo na mifumo mizuri ya elimu na afya, Iceland, Singapore, Finland, Estonia na Slovenia. Nyingine ni Cyprus, Belarus, Lukembourg , Norway na Korea Kusini.

Mwandishi: Sylvia Mwehozi/AFP
Mhariri: Yusra Buwayhid