WASHINGTON: Rais Bush aidhinisha sheria mpya ya ugaidi
18 Oktoba 2006Rais Geoge W Bush wa Marekani ameidhinisha sheria mpya dhidi ya ugaidi. Mswada wa sheria uliozusha utata unaliruhusu shirika la ujasusi la kimarekani, CIA, kuwahoji washukiwa wa ugaidi kutumia uwezo wake wote. Pia kesi za washukiwa zitasikilizwa katika mahakama za kijeshi.
Rais Bush amesema sheria hiyo ni muhimu kuzuia mashambulio mapya dhidi ya Marekani kama yale ya Septemba 11 mwaka wa 2001.
´Mswada huu unatoa usalama wa kisheria utakaohakikisha wanajeshi wetu na maofisa wa ujasusi hawatakuwa na haja ya kuogopa kushtakiwa mahakamani na magaidi kwa kufanya kazi yao.´
Wakosoaji na wataalmu wa sheria wamebashiri kuwa sheria hiyo mpya huenda ikafutiliwa mbali. Itawezesha kesi za washukiwa wa ugaidi kusikilizwa kwa haraka, ikiwa ni pamoja na wafungwa walio katika jela ya Guantanamo Bay nchini Cuba.