1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

WASHINGTON : Malengo ya kuongeza vikosi Iraq yatimizwa

13 Julai 2007
https://p.dw.com/p/CBjH

Rais George W. Bush wa Marekani ameitetea sera ya serikali yake ya kuongeza vikosi nchini Iraq kwa kusema kwamba malengo makuu ya sera hiyo yametimizwa.

Juu ya kwamba amesema bado kuna kazi kubwa ya kufanywa amesisitiza kwamba hakuna hatua itakayochukuliwa kuondowa vikosi hivyo kutoka Iraq.

Mkutano wa Bush na waandishi wa habari umefuatiwa na kutolewa kwa repoti ya muda iliokuwa ikisubiriwa kwa muda mrefu juu ya Iraq ambayo imegunduwa maendeleo yasio ya kuridhisha katika nyanja ya usuluhishi wa kisiasa nchini .

Bush amesema wale wanaoamini kwamba wameshindwa kwenye mapambano nchini Iraq yumkini wakataja utendaji usio wa kuridhisha katika baadhi ya malengo ya kisiasa na wale wanaoamini kwamba mapambano nchini Iraq yanaweza na lazima yashinde wanaona utendaji wa kuridhisha katika malengo kadhaa ya usalama kuwa sababu ya kuwa na matumaini.

Hata hivyo masaa machache baada ya kauli hiyo ya Bush Baraza la Wawakilishi limepitisha muswada wenye kutaka kuondolewa kwa vikosi vya wanajeshi wa Marekani kutoka Iraq kuanzia katika kipindi kisichozidi siku 120 na kumalizika hapo tarehe Mosi mwezi wa April mwaka 2009.

Baraza hilo la bunge limepiga kura 223 dhidi ya 201 kupitisha muswada huo kwa kumkaidi Rais Bush ambaye tayari ametumia kura ya turufu kupinga ratiba ya kuondowa vikosi kutoka Iraq ilioweka na chama cha Demokratik na ameahidi kutumia tena kura hiyo ya turufu kuzuwiya muswada huo.