1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

WARSAW : Kansela Merkel ziarani Poland

17 Machi 2007
https://p.dw.com/p/CCIH

Kansela Angela Merkel wa Ujerumani yuko nchini Poland kwa ziara ya siku mbili yenye lengo la kuboresha uhusiano uliodhoofika kati ya nchi hizo.

Katika hotuba kwa Chuo Kikuu cha Warsaw Merkel amesisitiza umuhimu wa kusonga mbele na katiba mpya ya Umoja wa Ulaya.Viongozi wawili wa Poland ambao ni ndugu mapacha Rais Lech Kaczynski na Waziri Mkuu Jaroslaw Kaczynski wana mashaka makubwa dhidi ya kufufuliwa kwa katiba hiyo ya Umoja wa Ulaya.

Merkel amelikwepa suala la mipango tata ya Marekani ya kutaka kuweka sehemu za makombora ya kujikinga nchini Poland na Jamhuri ya Czech.

Ujerumani ina wasi wasi juu ya Urusi kupinga vikali mipango hiyo na ametaka mzozo huo wa makombora ujadiliwe na Umoja wa Kujihami wa Mataifa ya Magharibi NATO.

Poland inasema inahitaji mkataba wa usalama na Marekani kwa sababu NATO haina azma ya kukabiliana na vitisho kutoka nchi kama vile Iran na Korea Kaskazini.