1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wapatanishi kuhusu mzozo wa Gaza kukutana tena Misri

Lilian Mtono
6 Aprili 2024

Wapatanishi kutoka Marekani na Israel wanatajiwa kukutana mjini Cairo kama sehemu ya msukumo mpya wa kufikia makubaliano ya kusitisha mapigano katika vita vinavyoendelea kati ya Israel na Hamas huko Gaza.

https://p.dw.com/p/4eUg6
Misri | Baerbock akizungumza na Sameh Shoukry
Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani Annalena Baerbock (kushoto) akiwa kwenye mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Misri Sameh Shoukry (wa pili kutoka kulia), pamoja na Waziri wa Mambo ya Nje wa Misri, wakikutana kwa majadiliano kuhusu mzozo wa Mashariki ya Kati.Picha: Christoph Soeder/dpa/picture alliance

Kabla ya mazungumzo hayo, Rais wa Marekani Joe Biden aliwarai viongozi wa Misri na Qatar kuwashinikiza zaidi Hamas kukubali na kuheshimu makubaliano, afisa mmoja mwandamizi ameliambia shirika la habari la AFP jana usiku.

Ikulu ya White House imethibitisha juu ya mazungumzo hayo, ingawa haikungumzia taarifa za vyombo vya habari vya Marekani kwamba Mkurugenzi wa Shirika la Ujasusi, CIA, Bill Burns, Mkuu wa Ujasusi wa Israel David Barnea, Waziri Mkuu wa Qatar Mohammed bin Abdulrahman Al-Thani na mkuu wa ujasusi wa Misri, Abbas Kamel pia watahudhuria.

Marekani, Qatar na Misri wamekuwa wakiratibu kwa miezi kadhaa sasa makubaliano ya kusitisha mapigano na kubadilishana mateka, ili upande mwingine wafungwa wa Kipalestina wanaozuiwa Israel waachiliwe. Hata hivyo mazungumzo hayo hayajazaa matunda tangu yale ya mwezi Novemba, ambayo yaliwezesha usitishwaji mapigano kwa muda wa wiki moja.