Wamisri waadhimisha mwaka mmoja wa mageuzi
25 Januari 2012Maelfu ya watu wenye itikadi kali ya Kiislamu, Waliberali, wenye itikadi ya mrengo wa shoto wameendelea kuongezeka katika uwanja wa kihistoria wa Tahrir baada ya mvua kubwa iliyonyesha usiku uliyopita ambayo watu wengi wameiita ni ishara ya neema.
Waandamanaji wamebeba magango yenye jumbe mbalimbali na nzito ambazo hazienadani au kuakisisi maana halisi ya mkusanyiko wa leo. Chama chenye nguvu kubwa ya kisiasa nchini humo, cha Udugu wa Kiislamu kipo katika maadhimisho hayo.
Mkusanyiko huu ni matunda ya kiini cha vuguvu kilichoanzia nchini Tunisia ambapo watu waliingia mitaani kushinikiza kuondoka madarakani kwa utawala wao.
Lakini tangu wakati huo makundi kadhaa, watetezi wa demokrasia waliokuwa wakishiriki harakati za mwaka uliyopita, wamekuwa wakisema kwamba jukumu lao halijakwisha na kwamba sasa hivi wanataka utawala wa kijeshi ambao umechukua hatamu ya uongozi baada ya kuondolewa madarakani Mubarak nao uondoke.
Bango kubwa la kwanza lililopo katika uwanja huo limeandikwa "Sherehe za maadhimisho ya kwanza" lingine limeandikwa "Chini, chini ya utawala wa kijeshi"
Majukwaa manee tofauti yamejengwa katika uwanja huo ambapo makundi tofauti yatapata fursa ya kupanda na kuwasilisha jumbe zao kwa umma wa Wamisri.
Swali kubwa lililoandikwa katika habari inayoongoza katika gazeti la serikali la Misri la kila wiki Al-Ahram linahoji " Nani atashikilia kiini cha mapinduzi ya Misri?"
Awali hapo jana Kiongozi Mkuu wa Kijeshi, Hussein Tantawi alitangaza kuiondoa kwa kiasi fulani sheria ya hali ya hatari ikionekana kama jitihada yake nyingine katika kuwatuliza waandamanaji.
Siku ambayo kitaifa nchini Misri ilijukana kama "Siku ya Polisi" Januari 25 hivi sasa Baraza Kuu la Kijeshi limeitangaza siku hiyo kuwa ni siku ya mageuzi ambapo shamra shamra za namna mbalimbali zitafanyika nchi nzima.
Vikosi vya usalama vipo katika mkao wa tahadhari kukabiliana hujuma yoyote yenye lengo la kuathiri sherehe hizo ingawa wizara ya mambo ya ndani ya nchi hiyo imesema hakutakuwa na polisi katika eneo ambalo waandamanaji wamekusanyika.
Jana shirika la haki za binadamu la Amnesty International lilitoa wito kwa mamlaka ya kijeshi nchini Misri kuwalinda waandamanaji na kuheshimu haki zao katika mkusanyiko huo wa amani.
Mwandishi: Sudi Mnette/AFP
Mhariri:Abdul-Rahman,Mohammed