Wamisri kupiga kura leo
28 Novemba 2010Wamisri wanapiga kura leo Jumapili huku kukiwa na ulinzi mkali katika uchaguzi wa bunge ambao unatarajiwa kukiimarisha chama tawala katika uongozi wa nchi hiyo na kudhoofisha kwa kiasi kikubwa upinzani wa makundi ya Kiislamu.
Idadi ya watu wanaotarajiwa kujitokeza kupiga kura katika nchi hiyo yenye wakaazi milioni 80 inakadiriwa kuwa ya chini , kutokana na hofu kwamba uchaguzi huo utafanyika huku wafuasi wa wagombea hasimu wakipambana na polisi baada ya kukamatwa kwa wapinzani 1,000 ambao ni wafuasi wa imani kali ya dini ya Kiislamu.
Vituo vya kupigia kura 254, vitafunguliwa asubuhi ya leo nchini kote, ambapo Wamisri milioni 40 wanahaki ya kupiga kura. Matokeo ya kwanza yanatarajiwa kuanza kutangazwa kesho Jumatatu.