1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wakenya walalamikia kuongezeka kwa ufisadi

16 Machi 2016

Utafiti Uliofanywa na taasisi ya serikali ya kupambana na rushwa Kenya inaonyesha kuwa nusu ya raia nchini humo wanaamini kuna ongezeko la matukio ya rushwa katika kipindi cha utawala wa rais Uhuru Kenyatta

https://p.dw.com/p/1IDzB
Kenia Garissa Universität Anschlag Kenias Präsident Uhuru Kenyatta äußert sich zu dem Anschlag
Picha: Reuters/Thomas Mukoya

Kulingana na taarifa hiyo, iliyotolewa na tume ya maadili na kupambana na rushwa, asilimia 74 ya idadi ya raia nchini humo , wanaamini kuwa rushwa imeongezeka katika utawala wa sasa wa rais Uhuru Kenyatta.

Tangu Rais Uhuru Kenyatta achukuwe madaraka April, 2013, mara kwa mara amekuwa kauli ya kukabiliana na rushwa na ufisadi nchini humo, wakati ambapo pia amekuwa akipata msukumo kutoka ndani na nje wa kumataka achukuwe hatua dhidi ya tatizo hilo sugu. Ingawa tayari amekwishawatimua mawaziri sita wa serikali yake waliohusishwa na tuhuma za ufisadi, wakosoaji wanasema bado hajafanya vya kutosha, wakati ambapo watuhumiwa wakuu zaidi wanaohusishwa na matukio hayo wakiendelea kuwa huru.

Mwenyekiti wa tume ya maadili Philip Kinisu amesema takriban Dola Bilioni 6, ambazo ni sawa na robo tatu ya bejeti ya nchi, zimebainika kupotea kwenye matukio yanayohusishwa na rushwa kwa mwaka. Kinisu aliyeanza kutumikia kito hicho mweyi Januari, amesema hivi karibuni tume yake hivi karibuni itawachunguza watumishi wake ili kuhakikisha kuwa hakuna anayejihusisha na rushwa.

Kwenye utafiti huo ambapo watu 5,260, kutoka kaunti 46 walihojiwa kwa siri, uliendeshwa kati ya mwezi Agosti na Oktoba na kubaini kuwa kati ya waliohojiwa asilimia 38 walishawahi kutoa rushwa kwenye taasisi mbalimbali za serikali katika kipindi cha mwaka jana. Wengi kati yao, walitoa rushwa wakati wakitafuta huduma za afya kwenye hospitali za serikali, ikifuatiwa na waliokuwa wakiomba vitambulisho vya uraia.

Barack Obama in Kenia mit Präsident Uhuru Kenyatta bei gemeinsamer Konferenz in Nairobi
Marekani inaitaka Kenya kupambana na kiwango kikubwa cha ufisadiPicha: Reuters/J. Ernst

Mwishoni mwa mwaka jana, Rais Kenyatta alitangaza rushwa kuwa tishio la usalama wa taifa. Taasisi ya kimataifa ya kupambana na rushwa- Trasparency International, kwenye ripoti yake ya mwaka 2015, iliitaja Kenya kuwa miongoni mwa nchi za mwisho, kwenye masuala ya uwazi ambapo ilikuwa ya 139 kati ya nchi 167.

Mwezi Novemba mwaka jana wakati akizindua mpango mkuu wa misaada ya dawa unaoratibiwa na Marekani, Balozi wa nchi hiyo nchini Kenya alisema jitihada zaidi zinahitajika katika kukabiliana na rushwa iliokithiri katika nchi hiyo ya Afrika Mashariki. Pia Rais wa Marekani Barack Obama wakati wa ziara yake nchini humo mwishoni mwa mwezi Julai mwaka jana, aliwataka Wakenya kujiendeleza kwa kuiondoa rushwa.

Ripoti hii inakuja muda mfupi baada ya shutuma zilizotolewa na rais Kenyatta dhidi ya raia wake kuhusina na masuala ya ufisadi. Akiwa ziarani huko Israel, Februari 25 mwaka huu, Alitoa shutuma hizo alipokuwa akizungumza na Wakenya wanaoishi nchini humo, akisema ni jambo la kusikitisha kwamba taifa la Kenya linasifika kwa mambo mabaya ikiwa pamoja na ufisadi uliokithiri, ukabila wa hali ya juu na matusi yanayoendelezwa hasa na wanasiasa.

Mwandishi: Lilian Mtono/AFP
Mhariri: Mohamed Abdul-Rahman