1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Wajerumani waadhimisha miaka 17 ya muungano

Oummilkheir3 Oktoba 2007

Viongozi kutoka sekta mbali mbali za kisiasa ,kiuchumi na kijamii wamemiminika Schwerin tangu asubuhi kuadhimisha sikuu kuu ya Muungano wa Ujerumani.Sherehe zimeanza kwa misa katika kanisa kuu la mjini Schwerin.

https://p.dw.com/p/CB0m
Rais Köhler kwenye sherehe mjini Berlin
Rais Köhler kwenye sherehe mjini BerlinPicha: AP

Viongozi kutoka sekta mbali mbali za kisiasa ,kiuchumi na kijamii wamemiminika Schwerin tangu asubuhi kuadhimisha sikuu kuu ya Muungano wa Ujerumani.Sherehe zimeanza kwa misa katika kanisa kuu la mjini Schwerin.

Sherehe rasmi zimeanza hivi punde katika ukumbi wa michezo ya kuigiza katika mji huo wa mashariki ya Ujerumani.

Mwenyeji wa sherehe za mwaka huu,waziri mkuu wa jimbo la Mecklenburg-Vorpommern,Harald Ringstorff,spika wa sasa wa baraza la wawakilishi wa majimbo-Bundesrat,amewakaribisha miongoni mwa wengineo rais wa shirikisho Horst Köhler,spika wa bunge la shirikisho Norbert Lammert,kansela Angela Merkel pamoja pia na mwenyekiti wa korti kuu ya katiba Hans Jürgen Papier. Mawaziri wakuu wa majimbo takriban yote ya Ujerumani na wawakilishi wa ofisi 100 za ubalozi wanahudhuria pia sherehe hizo.

Akizungumza na Radio Deutasche Welle,naibu spika wa bunge la shirikisho Bundestag Wolfgang Thierse ameelezea ufanisi uliopatikana miaka 17 tangu Ujerumani ilipoungana upya.

“Tangu mwaka 1990,haali imekua ikibadilika haraka kupita kiasi.Msimu wa kiangazi tuu, watu , na mie pia,walikua wakiamini utaratibu wa muungano utadumu miaka hadi utakapokamilika.Lakini ukosefu wa subira miongoni mwa jamii na shinikizo la kiuchumi lilikua kubwa kwa namna ambayo hali nzima ilibadilika haraka haraka.Na ni jambo la busara kwamba wanasiasa hawajasita sita,walikamilisha muungano.Muungano tuliutaka na ndio maana October tatu mwaka 1990 kwangu mie binafsi pia ni siku ya furaha.”

Sherehe za maadhimisho ya siku kuu ya Muungano wa Ujerumani zimeanza tangu jana kwa burudani ya muziki,densi,michezo ya kuigiza,filamu na spoti.Maelfu ya wananchi kutoka pande zote mbili za Ujerumani wanahudhuria sherehe hizo,kuadhimisha miaka 17 tangu walipoungana upya.

Kauli mbiu ya sherehe za mwaka huu ni “Ujerumani chini ya paa moja.”

Wakati huo huo kansela wa zamani Helmut Kohl ametunukiwa zawadi ya hesdhima kwa kufanikisha muungano.Rais wa zamani wa Marekani George Bush na kiongozi wa zamani wa Usoviet Michael Gorbatchov wamemsifu Dr.Helmut Kohl kwa juhudi zake za kurejesha muungano wa Ujerumani.Michael Gorbatchov amesema tunanukuu:kansela Helmut Kohl alikua kiongozi aliyefaa aliyekuwepo mahala panapofaa katika wakati muhimu kihistoria.

Hii ni mara ya pili kwa jimbo la Mecklenberg Vorpommern kuandaa sherehe za Muungano wa Ujerumani.Jimbo hilo la askazini mashariki limeshawahi kuandaa sherehe hizi mnamo mwaka 1992.