1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Vipi kuliokoa kampuni la Opel ?

18 Novemba 2008

Uchambuzi wa wahariri umetuwama zaidi leo juu ya jinsi ya kuliokoa Opel

https://p.dw.com/p/Fx94
Angela Merkel na vigogo vya General Motors (Ulkaya).Picha: AP

Uchambuzi katika safu za wahariri wa magazeti ya Ujerumani hii leo umetuwama mno juu ya mada moja:vipi kukiokoa kiwanda cha motokaa cha Opel nchini Ujerumani kisifilisike kutokana na msukosuko wa hatari ya kufilisika kiwanda mama cha Marekani cha General Motors ?

Hata jinsi Rais-mteule Barack Obama anavyoendesha shughuli zake wakati huu kabla kuapishwa rais Januari 20,mwakani kuligusiwa na gazeti la Ostthuringer Zeitung.

Ukimuangalia Obama unahisi yupo karibu nawe:Unamuhisi sasa ametulizana ,baridi kabisa na amejikomboa kutoka kampeni kali ya miaka 2 ya uchaguzi.Anaonekana tena mwenye mawazo na maarifa mengi ya nini la kufanya,mwerevu zaidi kuliko alivyoonekana katika kampeni zake nyingi.Anaruhusu kuulizwa maswali nyeti na ya shaka shaka...."

Hilo lilikuwa Ostthuringer Zeitung likitufungulia uchambuzi huu.Wahariri waliosalia wametuwama juu ya juhudi zinazofanywa humu nchini kuliokoa kampuni la magari la OPEL lisifilisike kutokana na msukosuko wa fedha nchini Marekani na athari zake ulimwenguni.Westfalenpost linalotoka Hagen laandika:

"Swali la kimsingi hapa linalofaa kuulizwa: je, serikali inafaa kuliokoa kampuni kifedha ili lisifilisike ? Jibu lake ni rahis:la ,hasha.Kuna swali jengine ikiwa haifai kufanya hivyo: Je, serikali itamdu kutumbua macho tu kuliachia kampuni la Opel kufilisika ikiwa hii itaongoza kupoteza maalfu nafasi zao za kazi ? Au kuviathiri viwanda vidogo vinavyotoa vipurii kwa kampuni hilo ?Hata ikiwa si haki mbele ya viwanda vingi vidogo vidogo-la hasha serikali haiwezi .

Ni athari za kufilisika kwa kiwanda cha Opel kwa wengine wasiohusika moja kwa moja ndiko kunakostahiki serikali kuingilia kati na kuliokoa kwa msaada wa dharura.

Kufanya hivyo lakini ni kukiuka muongozo wa Umoja wa Ulaya wa kuwapo mashindano huru kati ya viwanda.Bila kujali msaada kama huo utachukua sura gani,utapiga mfano wa kuja kufuatwa baadae." Matokeo yake-laandika gazeti-yule anaelitia jeki kulisaidia kampuni la magari la Opel, huyu hawezi kulikatalia msaada kampuni la magari la FORD.

Kudai mwanasiasa yeyote wa Ujerumani siku za nyuma kuwa kampuni la Opel litaifishwe, mwanasiasa huyo angeitwa "raia wa heshima kutoka Kuba".

Kuwa wazo hilo linazkngatiwa kunadhihirisjha kwamba msukosuko wa uchumi uliozuka kwa kasi mno umeibua ukweli mpya kwenye masoko .Dai hilo la kutaifisha si la kipumbavu hivyo kama linavyoonekana kwanza: Katika kesi ya Opel na kutokana na yale mtu anayojua,Opel halikuongozwa vibaya na hivyo halifai kampuni hili kutupwa katika jaa la takataka za ubepari..."

Gazeti la Neue Ruhr/Neue Rhein-Zeitung linadai Kampuni la Opel huko Russelsheim halikofanya madhambi yoyote kusababisha msukosuko wa fedha uliozuka kwa kuwa tu limeingizwa katika balaa lililolikumba kampuni mama la GM au General Motors nchini Marekani.Gazeti laongeza:

"Kwahivyo inafaa sana kwa serikali ya ujerumani kuzingatia barabara vipi kulisaidia.Ikiwa Opel haina makosa,wafanyakazi wa kiwanda hiki cha magari wanastahiki kuokolewa.Kwani, jambo moja ni dhahiri-shahiri kilio cha kuomba msaada kutoka serikali kuu mjini Berlin kitazidi kuhanikiza.

Serikali lakini imeshajitolea kutoa Euro bilioni 500 kuyasaidia mabanki humu nchini.Sasa serikali ina hatari ya kujitwika mzigo mkubwa zaidi isiouweza.

Msaada zaidi kutoka hazina ya serikali sio tu hautasaidia kuokoa mambo bali hauwezi pia kugharimiwa."

Katika hali hii serikali inabakiwa na chaguo moja kati ya maovu mawili:

Latumalizia gazeti la Volksfreund kutoka Trier:

Ama serikali inalisaidia kampuni la Opel na kujua kwamba baadae viwanda vyengine kama Volkswagen au Ford vitapiga hodi katika afisi ya Kanzela kuomba msaada au serikali haijiingizi kati na kuwa tayari kujionea athari zake kubwa za kuporomoka viwanda vidogovidogo vyenye kutengeza vipuri kwa viwanda hivyo vikubwa na kuongezeka mno kwa ukosefu wa kazi nchini.Si ajabu mkutano wa jana wa kilele kwa Kanzela Angela Merkel haukupitisha uamuzi wazi.