1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Upatanisho sio Kisasi

K.Küstner - (P.Martin)13 Februari 2009

Mji wa Ujerumani Dresden unajulikana kote duniani ukihusishwa na Vita Vikuu vya Pili na jinsi ulivyoteketezwa wakati wa vita hivyo.

https://p.dw.com/p/GtGF
Ruinen in Dresden / Foto 1945 2. Weltkrieg/ Alliierte Luftoffensive gegen d. Reichsgebiet/ Bombardierung der Stadt Dresden am 14./15. Februar 1945. Nach dem Angriff liegen 20 Qua- dratkilometer der Stadt in Schutt und Asche. - Blick vom Rathausturm auf die Ruinen der Dresdener Innenstadt. - Foto
Mji wa Dresden baada ya kushambuliwa Februari 1945 katika Vita Vikuu vya Pili .Picha: picture-alliance / akg-images

Usiku wa tarehe 13 kuamkia 14 Februari mwaka 1945,mji huo uliteketezwa katika mashambulizi ya bomu yaliyofanywa na mataifa shirika.Watu 25,000 waliuawa. Kila mwaka Februari 13,wakaazi wa Dresden hukumbuka mashambulio ya usiku huo.Lakini tangu miaka michache iliyopita,mafashisti mamboleo pia huitumia siku hiyo kufanya maandamano yao wenyewe. Lakini wakaazi wa Dresden wanataka kukomesha mtindo huo.Muandishi wetu Cornelia Kästner anaeleza zaidi katika ripoti inayosomwa studioni na Prema Martin.

Mkaazi wa Dresden Nora Lang anajua maana ya vita,kwani yeye ni miongoni mwa wale walionusurika usiku wa Februari 13 mwaka 1945. Wakati huo Nora Lang alikuwa na miaka 13 na hadi hii leo anaikumbuka vizuri siku hiyo kwani ilikuwa siku ya kanivali.Watoto walifurahia siku hiyo mitaani,lakini wakati wa jioni mji wa Dresden ulishambuliwa kwa mara ya kwanza.Mtaa wa Johannstadt alikoishi Nora Lang wakati huo uliteketezwa kabisa.Anasema hadi hii leo anaiona picha hiyo mbele ya macho yake.

"Wakati huo nilihisi kuwa ni mwisho wa dunia.Lilipotokea shambulio la pili nilitengana na wazazi wangu na kaka yangu.Sina maneno ya kueleza shambulio hilo la pili."

Nora Lang na mdogo wake waliotengana na familia baada ya shambulizi la pili walifanikiwa kuukimbia mji ulioteketezwa.Hata familia yake ilinusurika usiku huo wa mashambulizi ya bomu.Lakini maelfu ya watu walipoteza maisha yao katika janga hilo la moto.

Kila mwaka tarehe 13 Februari wakaazi wa Dresden huwakumbuka wale waliopoteza maisha yao na huombea upatanisho na vita vyote kumalizika. Lakini tangu miaka michache iliyopita kumbukumbu hiyo inatiwa dosari za chuki na makundi ya sera kali za mrengo wa kulia.Wafuasi wake hufanya kile wanachokiita maandamano ya huzuni huku wakibeba mabango yanayosema "Hakuna Msamaha". Mwaka huu kama mafashisti mamboleo 8,000 wanatazamiwa kuandamana-hiyo ikiwa ni idadi kubwa mno ikilinganishwa na miaka iliyopita.

Anetta Kahane wa Amadeu Antonio Stiftung- taasisi inayopinga sera kali za mrengo wa kulia anasema,si tu vijana wa Kijerumani waliochanganyikiwa akili,wanaopotoshwa na mafashisti.Anasema,hayo ni maandamano ya mafashisti mamboleo barani Ulaya.Makundi hayo yote hukusanyika Dresden na huchaguliwa kama mji wa kihistoria kuonyesha umoja wao. Mtindo huo ni hatari.Lakini baadhi kubwa ya wakaazi wa Dresden wanataka upatanisho sio kisasi.Kwa kushirikiana kidemokrasia,wakaazi wa Dresden wanataka kuonyesha kuwa maandamano ya mafashisti mambo leo hayafanywi kwa niaba yao.